Taratibu za ibada 
NJONI TUABUDU: TARATIBU ZA IBADA       (KWA MAKANISA YA KIPRESITERI) [1, 1 ed.]
 97899768845093

Table of contents :
YALIYOMO
TABARUKU i
Imani ya Mitume ii
Sala ya Bwana ii
Baraka ii
Imani ya Nikea (AD 325) iii
UTANGULIZI iv
YALIYOMO vi
I. IBADA YA JUMAPILI 1
Viongozi wa ibada ya Jumapili 1
Utaratibu wa Ibada ya Jumapili 6
II. IBADA ZA SAKRAMENTI 11
1. Ibada ya Ubatizo 11
2. Ibada ya Meza ya Bwana 18
III. IBADA ZA MAOMBI 25
1. Ibada ya Maombi ya Ki-Danieli 25
2. Ibada ya Maombi ya Jumatano 26
3. Ibada ya Maombi ya Ijumaa 27
4. Ibada ya Maombi ya Idara 28
5. Ibada ya Maombi ya Kifamilia 28
Taratibu za ibada za Maombi 29
IV. IBADA ZA KISHEREHE 30
1. Ibada ya Ndoa 30
2. Ibada ya Mazishi 39
3. Ibada ya Kusimika Wachungaji 45
4. Ibada ya Kusimika Wazee wa Kanisa 49
5. Ibada ya Kuingiza Watumishi Kazini 53
6. Ibada ya Kutoa kibali cha kuhubiri (Leseni) 55
7. Ibada ya Kuweka Wakfu Jengo 58
8. Kuweka Wakfu Vifaa vya Kanisa 64
9. Ibada ya Mahafali ya Chuo cha Biblia 66
10. Ibada ya Mahafali ya Shule ya Awali, Msingi na Sekondari 70
V. IBADA ZA SIKUKUU ZA KANISA 74
1. Ibada ya Siku ya Kwanza ya Mwezi 74
2. Ibada ya Krismasi 75
3. Ibada ya Mwaka Mpya 75
4. Ibada ya Pasaka 76
5. Ibada ya Jumapili ya Siku ya Matengenezo 76
Utaratibu wa ibada Jumapili ya Siku ya Matengenezo 77
VI. IBADA ZA IDARA ZA KANISA 81
1. Juma la Wanawake 81
2. Juma la Wanaume 81
3. Juma la Vijana 82
4. Juma la Watoto 82
Utaratibu wa Ibada za Idara 83
VIFUNGU VYA MSAADA 86
Kuhusu Ibada ya Jumapili; Zaburi. 86
Kuhusu Ibada ya Ubatizo 86
Kuhusu Ibada Meza ya Bwana 87
Kuhusu Ibada ya Maombi 87
Kuhusu Ibada ya Ndoa 87
Kuhusu Ibada ya Mazishi 88
Kuhusu Ibada ya Kusimika Wachungaji 88
Kuhusu Ibada ya Kutoa Kibali Cha Kuhubiri (Leseni) 88
Kuhusu Ibada ya Kuweka Wakfu Jengo 88
Kuhusu Ibada ya Kuwekwa Wakfu Vifaa 89
Kuhusu Ibada ya mahafali ya shule/vyuo 89
Kuhusu Ibada ya Siku ya kwanza ya Mwezi na Mwaka Mpya 89
Kuhusu Ibada ya Krismasi 89
Kuhusu Ibada ya Pasaka 89
Kuhusu Ibada ya Jumapili ya Matengenezo 90
Kuhusu Juma la Wanawake 90
Kuhusu Juma la Wanaume 90
Kuhusu Juma la Vijana 91
Kuhusu Juma la watoto 91
Kielelezo A. Mpangilio wa Mkao Kanisani 92

Citation preview

NJONI TUABUDU

TARATIBU ZA IBADA

PRESBYTERIAN CHURCH 2

Hakimiliki © 2020 Daniel John Seni Chapa ya Pili, 2020

Msanifu: Eternal Word and Charity Publishing (EWCP) Dar es Salaam [+255-755-643-590] Mchapaji: Truth Printing Press. Dar es Salaam [+255764425704] ___________________________________ Haki zote zimehifadhiwa. Hakuna sehemu ya chapisho hili inayoweza kuzalishwa tena, au kuboreshwa au kusambazwa kwa njia yoyote au kwa kubadilisha umbo au kunakili na kupeleka katika umbo linwa gine bila idhini ya maandishi ya mchapishaji, isipokuwa kwa nukuu fupifupi kwa matumizi yasiyo ya kibiashara. Kwa maombi ya ruhusa, tuma ujumbe kwa msambazaji, ukianza na neno “Tahadhari” bila kusahau ISBN ya toleo hili.

Maandiko ya Biblia yamechukuliwa kutoka kwenye Biblia ya Kiswahili Toleo la shule inayotolewa na Swahili Union Version (SUV).

________________________ Msambazaji Shekinah Mission Centre (SMC) [email protected] S.L.P 32807 Dar es Salaam +255 769 080 629 +255 787 907 347 Madale/Mivumoni, Joshua road, mkabala na Shule ya Msingi-Atlas/ at Shekinah Presbyterian Church in Tanzania, Dar es Salaam

TABARUKU

Kwa Watumishi wote katika Makanisa ya Kipresbiteri

i

Imani ya Mitume Namwamini Mungu Baba Mwenyezi, Muumba wa Mbingu na Nchi, Na Yesu Kristo Mwana Wake Pekee, Bwana Wetu, aliyechukuliwa mimba kwa Uwezo wa Roho Mtakatifu, Akazaliwa na Bikra Mariamu, Akateswa zamani za Pontio Pilato, Akasulubiwa, Akafa, Akazikwa, Akashuka mahali pa wafu, siku ya tatu Akafufuka, Akapaa mbinguni, Ameketi mkono wa Kuume wa Mungu Baba Mwenyezi, Kutoka huko atakuja kuwahukumu walio hai na wafu. Namwamini Roho Mtakatifu, Kanisa Takatifu lililo moja, Ushirika wa Watakatifu, Ondoleo la dhambi, kiyama ya mwili na uzima wa milele. Amina.

Sala ya Bwana Baba yetu uliye mbinguni, Jina lako litukuzwe, ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni, utupe leo riziki yetu, utusamehe makosa yetu, kama nasi tunavyowasamehe waliotukosea, usitutie majaribuni, bali utuokoe na yule mwovu, kwa kuwa ufalme ni wako, na nguvu, na utukufu na hata milele. Amina.

Baraka Neema ya Bwana Wetu Yesu Kristo, na Upendo wa Mungu Baba, na Ushirika wa Roho Mtakatifu, ukae nanyi nyote sasa na hata milele.” Amina ii

Imani ya Nikea (AD 325) Tunamwamini Mungu mmoja Baba, Mwenyezi, Muumba wa Mbingu na Nchi, na vitu vyote vinavyoonekana na visivyoonekana. Tunamwamini Bwana mmoja, Yesu Kristo, Mwana wa pekee wa Mungu, mzaliwa wa milele wa Baba, Mungu kutoka kwa Mungu, Nuru kutoka kwa Nuru, Mungu wa kweli kutoka kwa Mungu wa kweli, aliyezaliwa, lakini hakuumbwa, ni nafsi moja na Baba. Kupitia yeye vitu vyote viliumbwa. Kwa ajili yetu na kwa ajili ya wokovu wetu alishuka kutoka mbinguni; kwa nguvu za Roho Mtakatifu alichukua mwili kutoka kwa Bikira Mariamu, na akafanywa mwanadamu. Kwa ajili yetu alisulubiwa chini ya Pontio Pilato; akafa na akazikwa. Siku ya tatu akafufuka tena kama yasemavyo Maandiko; akapaa mbinguni na ameketi mkono wa kuume wa Baba. Atakuja tena katika utukufu kuhukumu walio hai na wafu, na ufalme wake hautakuwa na mwisho. Tunamwamini Roho Mtakatifu, Bwana, mpaji wa uzima, ambaye anatoka kwa Baba na Mwana. Pamoja na Baba na Mwana huabudiwa na kutukuzwa. Amezungumza kupitia Manabii. Tunaamini kanisa moja, takatifu, la ulimwenguni pote, na la kitume. Tunakubali ubatizo mmoja kwa msamaha wa dhambi. Tunatazamia ufufuo wa wafu, na maisha ya ulimwengu ujao. iii

UTANGULIZI Ibada ndilo jambo la muhimu sana katika maisha ya kanisa. Mambo yote ambayo kanisa linafanya kwa ajili ya kumtukuza Mungu yanaweza kufanyika kama sehemu ya ibada. Ibada huonesha namna jamii ya waaminio wanavyojibu mwitikio wao kwa Mungu. Ibada ni tendo la rohoni, kwa hiyo kila mmoja lazima aandae moyo wake; hata hivyo, kukusanyika mahali na kumwabudu Mungu ndilo tendo la wazi linaoonesha imani yetu kwa Mungu. Katika ibada, tunaungana na Kristo kama mtu mmoja. Kupitia ibada, kanisa linatiwa nguvu katika kumtumikia Mungu katika ulimwengu huu. Katika Imani ya Westminister, Sehemu ya 7 tunasoma hivi; “Ni sheria ya maisha yetu ya asili na ya kidunia kutenga muda fulani kwa ajili ya ibada kwa Mungu.” Ikumbukwe kwamba katika Biblia hakuna utaratibu maalum wa ibada, hata hivyo kanisa kwa hekima linaandaa miongozo mbalimbali kwa ajili ya kuhakikisha kwamba watu wanamwabudu Mungu katika hali ya ubora. Utaratibu mzuri wa ibada hutusaidia kumwabudu Mungu kwa uzuri na utakatifu na kisha kumrudishia utukufu. Pia utaratibu mzuri wa ibada hufanya washirika ndani ya ibada kushiriki kikamilifu katika mazoezi yote yanayofanyika katika ibada husika. Ni wito iv

wangu kwa wote watakaotumia utaratibu huu kumwomba Roho Mtakatifu ili kufanya ibada iwe hai ndani ya kanisa. Ingawa tunatumia utaratibu wa ibada kuongoza ibada kanisani, lakini ukweli ni kwamba Roho Mtakatifu huongoza ibada zetu. Tunapokuwa tunafanya ibada kwa uaminifu, ndipo tutasikia sauti ya Mungu ya mwito wetu. Katika Matendo ya Mitume 13:2 tunasoma, “walipokuwa wakimfanyia Bwana ibada na kufunga, Roho Mtakatifu akasema Nitengeeni Barnaba na Sauli kwa kazi niliyowaitia.” Hawa walisikia sauti ya Roho Mtakatifu moja kwa moja kwa sababu walikuwa wakimfanyia Mungu ibada. Neno la Mungu pia linasema, “Mungu ni Roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli” (Yn. 4:24). Kitabu hiki kimeandaliwa kwa ajili ya kuwasaidia watumishi wa Mungu katika huduma zao. Katika kitabu hiki kuna taratibu za ibada karibu zote zinazojulikana na mwishoni kuna vifungu vya Biblia kuhusiana na ibada husika.

Wenu. Daniel John Seni Shekinah Presbyterian Church Tanzania Dar es Salaam Novemba, 2020. v

YALIYOMO TABARUKU ................................................................... i Imani ya Mitume .......................................................... ii Sala ya Bwana ............................................................. ii Baraka ......................................................................... ii Imani ya Nikea (AD 325) .............................................. iii UTANGULIZI ............................................................... iv YALIYOMO .................................................................. vi I. IBADA YA JUMAPILI ............................................ 1 Viongozi wa ibada ya Jumapili ..................................... 1 Utaratibu wa Ibada ya Jumapili ................................... 6 II. IBADA ZA SAKRAMENTI .................................... 11 1. Ibada ya Ubatizo ................................................ 11 2. Ibada ya Meza ya Bwana.................................... 18 III. IBADA ZA MAOMBI ........................................... 25 1.

Ibada ya Maombi ya Ki-Danieli ............................................ 25

2.

Ibada ya Maombi ya Jumatano ........................................... 26

3.

Ibada ya Maombi ya Ijumaa .................................................. 27

4.

Ibada ya Maombi ya Idara ..................................................... 28

5.

Ibada ya Maombi ya Kifamilia .............................................. 28

Taratibu za ibada za Maombi...................................... 29 IV. IBADA ZA KISHEREHE ...................................... 30 1. Ibada ya Ndoa ................................................... 30 2. Ibada ya Mazishi................................................ 39 3. Ibada ya Kusimika Wachungaji .......................... 45 4. Ibada ya Kusimika Wazee wa Kanisa ................. 49 5. Ibada ya Kuingiza Watumishi Kazini .................. 53 6. Ibada ya Kutoa kibali cha kuhubiri (Leseni) ....... 55 7. Ibada ya Kuweka Wakfu Jengo .......................... 58 8. Kuweka Wakfu Vifaa vya Kanisa ........................ 64 9. Ibada ya Mahafali ya Chuo cha Biblia ................ 66 vi

10. Ibada ya Mahafali ya Shule ya Awali, Msingi na Sekondari .................................................................. 70 V. IBADA ZA SIKUKUU ZA KANISA ........................ 74 1.

Ibada ya Siku ya Kwanza ya Mwezi .................................... 74

2.

Ibada ya Krismasi ..................................................................... 75

3.

Ibada ya Mwaka Mpya ............................................................ 75

4.

Ibada ya Pasaka ........................................................................ 76

5.

Ibada ya Jumapili ya Siku ya Matengenezo .................... 76

Utaratibu wa ibada Jumapili ya Siku ya Matengenezo 77 VI. IBADA ZA IDARA ZA KANISA ............................. 81 1. Juma la Wanawake..................................................................... 81 2.

Juma la Wanaume ................................................................... 81

3.

Juma la Vijana .......................................................................... 82

4.

Juma la Watoto ......................................................................... 82

Utaratibu wa Ibada za Idara ....................................... 83 VIFUNGU VYA MSAADA ............................................. 86 Kuhusu Ibada ya Jumapili; Zaburi. ............................... 86 Kuhusu Ibada ya Ubatizo .............................................. 86 Kuhusu Ibada Meza ya Bwana ..................................... 87 Kuhusu Ibada ya Maombi .............................................. 87 Kuhusu Ibada ya Ndoa .................................................. 87 Kuhusu Ibada ya Mazishi .............................................. 88 Kuhusu Ibada ya Kusimika Wachungaji ....................... 88 Kuhusu Ibada ya Kutoa Kibali Cha Kuhubiri (Leseni) ... 88 vii

Kuhusu Ibada ya Kuweka Wakfu Jengo ....................... 88 Kuhusu Ibada ya Kuwekwa Wakfu Vifaa ..................... 89 Kuhusu Ibada ya mahafali ya shule/vyuo .................... 89 Kuhusu Ibada ya Siku ya kwanza ya Mwezi na Mwaka Mpya .............................................................................. 89 Kuhusu Ibada ya Krismasi ............................................ 89 Kuhusu Ibada ya Pasaka .............................................. 89 Kuhusu Ibada ya Jumapili ya Matengenezo .................. 90 Kuhusu Juma la Wanawake .......................................... 90 Kuhusu Juma la Wanaume ............................................ 90 Kuhusu Juma la Vijana.................................................. 91 Kuhusu Juma la watoto ................................................. 91 Kielelezo A. Mpangilio wa Mkao Kanisani ..................... 92

viii

I.

IBADA YA JUMAPILI

Siku ya Jumapili ndiyo siku ya Ibada Kuu. Kimaandiko ndiyo siku ya Kwanza ya Juma, na ndiyo siku ya Sabato ya Kikristo. Wakristo wanapaswa kujiandaa mapema kwa ajili ya siku hii muhimu kwa ajili ya kumwabudu Mungu.

Viongozi wa ibada ya Jumapili Kwa kawaida, ibada zetu zinakuwa na viongozi watatu ambao wanahusika moja kwa moja katika kuongoza ibada husika: a) kiongozi wa ibada b) mwombaji c) mhubiri. Hawa wote wanapaswa kuwa na mawasiliano ya karibu katika kuhakikisha kwamba ibada inafanyika katika hali ya utaratibu. a)

Kiongozi wa Ibada Ingawa Mkristo yeyote anaweza kuongoza ibada ya Jumapili, inapendekezwa kwamba mojawapo ya watu wafuatao wawe waongoze ibada; Mchungaji, Mzee, Shemasi na Mwinjilisti. Hata hivyo, kama hawa watu wote hawapo; kwa mfano kama kanisa bado changa au limeanzishwa hivi karibuni, basi mtu yeyote anaweza kuongoza ibada. 1

Kabla ya Ibada Mara unapokuwa umetangazwa kuwa kiongozi wa ibada, hakikisha mambo yafuatayo unayazingatia haraka iwezekanavyo; 1) Unapaswa kujua ni nani ambaye atahubiri siku hiyo, na baada ya kujua unapaswa kuwa na andiko la mahubiri ya siku hiyo. 2) Unapaswa kujua ni nani atakayeongoza maombi siku hiyo. 3) Unapaswa kujua ni kwaya gani itakayoimba siku hiyo. 4) Unapaswa kujua ni nyimbo gani za vitabuni zitaimbwa siku hiyo (Nyimbo hizo ziendane na mahubiri ya siku hiyo). 5) Unapaswa kujua ni wazee au mashemasi gani walio katika zamu kwa siku hiyo. 6) Unapaswa kujua ni akina nani watasafisha, na kuandaa mazingira (usafi wa ndani na mapambo ndani ya kanisa) Ndani ya ibada a) Unapaswa kuingia mapema ndani ya kanisa. Angalau dakika kumi kabla ya ibada kuanza. b) Epuka kuongea maneno mengi kama mshereheshaji

2

c) Epuka kupokea matangazo ya dharura. Au kama ni lazima sana, hakikisha unawasiliana na mchungaji kwa haraka. d) Unapaswa kujua kuwa Mungu anaenda kukutumia katika ibada hiyo; basi hakikisha kwamba unafanya kila kitu kwa utaratibu mzuri. e) Hakikisha unapanga mtu wa kuhesabu washirika wa siku hiyo; f) Chagua Zaburi ya Kusoma wakati wa kuanza ibada mapema (Rejea Uk 88) Baada ya ibada a) Hakikisha unatoa tathmini nzuri pamoja na viongozi wengine baada ya ibada; b) Hakikisha mnajaza vitabu vya kanisa vinavyohusu mahudhurio na matoleo. c) Kama ni mzee au shemasi, basi unawajibika moja kwa moja katika kuhesabu matoleo ya siku hiyo. b) Mwombaji Mwombaji ni mtu ambaye anawakilisha maombi kanisani. Anasimama kwa ajili ya kuomba kwa niaba wa waabudu wengine. Mwombaji anapaswa kuandaliwa mapema (mara nyingi anapaswa kusomwa Jumapili katika matangazo ya ujumla 3

kama viongozi wengine). Ushauri kwa mtu yeyote anayetajwa kuomba: a) Anapaswa kujiandaa kwa kumwomba Mungu kabla hajaenda kuomba mbele ya watu wengine. b) Ingawa anamwomba Mungu, ukweli ni kwamba watu wanaosikiliza wanabarikiwa na maombi yake, na kupata neema mioyoni mwao; hivyo ni lazima aweze kutamka maneno vizuri na kwa usahihi. c) Kama hana uzoefu wa kuomba mara nyingi mbele ya watu, basi ni muhimu kufanya mazoezi; ikiwa ni pamoja na kuandika maneno yote ambayo ataomba; kuandika maneno haimaanishi kwamba tunapingana na mwongozo wa Roho Mtakatifu (kwa sababu yeye hata kabla hatujaomba ameshajua) bali ni kuwa tayari na kutokuwakwaza watu wengine ambao watasikiliza maombi yetu. d) Kama utaona shida kuandika, basi andika hata pointi ambazo utaenda kuomba; na utakuwa unaziangalia moja baada ya nyingine. e) Tumia angalau dakika 2-4 kuongoza maombi haya. Kwa sababu umeandaliwa kwa muda mrefu, basi tumia kwa usahihi muda huo kwa ajili ya kumtukuza Mungu. 4

f) Hakikisha unakuwa na maombi yaliyo sahihi kimaandiko. g) Epuka kuhubiri kwenye maombi yako au kuwasilisha ujumbe fulani kwa watu kupitia maombi. h) Epuka kulaumu watu kwenye maombi yako (mfano wachelewaji, wazembe nk) i) Ukiomba toba, epuka kutaja dhambi moja moja, bali sema kwa ujumla tu. j) Omba kwa lugha inayoeleweka ambayo waamini wengine watasikiliza na kuelewa. c) Mhubiri Mhubiri ni mtu muhimu katika ibada. Mojawapo ya alama za kanisa la kweli ni Kuhubiriwa kwa neno la Mungu kwa usahihi. Mhubiri anapaswa kujua yafuatayo; a) Lazima ajue kwamba atatumia muda gani katika mahubiri yake b) Lazima aende na wakati. Kama ukiona ratiba zinaingiliana sana na muda umeenda sana, si lazima uhubiri kila kitu. c) Unapaswa kujua kwamba ingawa utaeleza mambo mengi sana, lakini watu watachukua machache tu. Hivyo basi hakikisha unazingatia muda na unakuwa mtu anayebadilika. 5

d) Kuwa makini, usicheze na roho za watu minbarini kwa kuwadharau kwa hali zao nk. e) Mwisho wa mahubiri ita watu kwa Bwana kama sehemu ya mwitikio wa ujumbe. f) Kama ni mchungaji mwisho wa ibada utapaswa kutoa baraka kwa kanisa. (Zingatia ni mwisho wa ibada)

Utaratibu wa Ibada ya Jumapili Maelekezo: Inapendekezwa kwamba ibada ya Jumapili ifanyike kwa muda usiozidi saa mbili (2), hata hivyo, kwa kuzingatia kanisa liko wapi, na watu wakoje, wanaweza kuamua kuzidisha muda; kwani hatufungwi na muda wa kumwabudu Mungu. Watu wasio na jukumu lolote; hata kama wakiwa ni viongozi wa kanisa wasikae mbele isipokuwa kama wana majukumu maalum ndani ya ibada. Hata kama ni mchungaji kama hana jukumu lolote hapaswa kukaa mbele; Na hata yule mwombaji akimaliza zamu yake anapaswa kurudi na kukaa nyuma. Hata hivyo viti vya viongozi lazima vikae mstari wa mbele. (Rejea 95)

Mtiririko wa Ibada ni kama ifuatavyo: 6

Maelekezo: Mwanzoni mwa ibada wataanza kwa nyimbo za kusifu na kuabudu kwa muda wowote ambao kanisa limekubaliana. Ikumbukwe kwamba huu ni mwongozo tu ambao kiongozi anapaswa kufuata, lakini haimaanishi kwamba hawezi kuweka vionjo kwa kuzingatia mazingira.

Kiongozi: Basi ndugu zangu baada ya kusifu na kuabudu, tutulie mbele za Mungu muda huu, Biblia inasema “Bwana yupo ndani ya hekalu lake takatifu; dunia yote na inyamaze kimya mbele zake” (Habakuki 2:20) na tuombe sala ya toba katika hali ya kimya mbele za Bwana. Tukiwa katika hali ya kusimama Washirika: (kila mmoja ataomba kimoyomoyo) Kiongozi: (soma zaburi kisha uombe: huhitaji kusema unasoma zaburi namba ngapi. Rejea Uk. 85) Tuombe Kiongozi: Tukiwa katika hali ya kusimama tukiri imani ya mitume inayotuunganisha na Wakristo wengine ulimwenguni. Washirika: Amina Kiongozi: Nawasihi tukae na tuimbe wimbo namba…….. 7

Kiongozi: Naomba mtu aliyeandaliwa kwa ajili ya maombi aombe. Kiongozi: Huu ni wakati wa kusoma neno la Mungu ambalo litatuongoza katika mahubiri ya leo. Kiongozi: Huu ni muda wa kumsifu Mungu kupitia kwaya! Karibuni wanakwaya. Kiongozi: Huu ni muda wa kusifu na kuabudu. Baada ya kusifu na kuabudu tutaomba kwa pamoja. Maelekezo: Ni vizuri kwa kila kanisa kuandaa kikundi maalum cha kusifu na kuabudu ambacho ndicho kitakachohusika na shughuli zote za nyimbo kanisani.

Kiongozi: Huu ni wakati wa kusikiliza neno la Mungu kutoka kwa…………. Maelekezo: Mhubiri atahubiri kwa muda usiozidi dakika 40. kama ataona kwamba kuna uhitaji wa kuwaita watu kumpokea Yesu Kristo kuwa Bwana na Mwokozi wa maisha yao atawaita wakati huo huo. Kama asipofanya hivyo, kiongozi wa ibada lazima aite watu wenye shida mbalimbali kwa ajili ya kuombewa. Vile vile unaweza kuwataka waumini wote kuomba 8

kwa pamoja kama mwitikio kwa Neno la Mungu.

Kiongozi: Ni wakati wa kutoa sadaka. Wakati huu kwaya itaimba wimbo/nyimbo……… Kiongozi: Ni wakati wa kusikiliza matangazo ya leo. Namkaribisha asome Matangazo ya leo. Maelezo: katika matangazo hakikisha wageni wanatambulishwa. Muda huu unaweza kutumika pia kwa ushuhuda.

Kiongozi: Tusimame namba_

sote

Kiongozi: Ni wakati Mungu.

wa

na

tuimbe

kupokea

wimbo

baraka

za

Maelekezo: Mchungaji atainua mikono yake yote kwa washirika na kutamka; mwinjilist au mleseni hapaswi kufanya. Kama Mchungaji hayupo ni sala ya Bwana.

Kiongozi: Tutoke kwa utaratibu maalum (kikundi cha kumsifu na kuabudu au kwaya wanaweza kuongoza nyimbo wakati wa kutoka)

Maelekezo:

Utaratibu wa kutoka ni kwamba atatangulia Kiongozi wa ibada, Mhubiri, na kisha Mwombaji na watajipanga kwa mtiririko 9

huo na kisha watafuatia.

waumini

wengine

wote

Kiongozi: Kila mmoja amtakie mwenzake baraka za Mungu “nakutakiwa baraka za Mungu ziwe pamoja nawe” kwa kila mmoja kumshika mkono mwenzake. Unaweza kushika watu wengi kwa kadri uwezavyo. Kiongozi: Asanteni kwa kushiriki ibada ya leo, naomba kila mtu awe na angalau dakika moja ya kuzungumza na mwenzake na kutiana moyo.

10

II. IBADA ZA SAKRAMENTI Tunazo Sakramenti mbili tu: Ubatizo na Meza ya Bwana. Taratibu zifuatazo zitazingatiwa kulingana na mazingira husika

1. Ibada ya Ubatizo Maelekezo: Ubatizo huweza kufanyika siku yoyote ile endapo kuna hitaji la kufanya hhivo. Wale wanaobatizwa wanapaswa kuandaliwa mapema ikiwa ni watu wazima wanapaswa wawe wameshapokea mafundisho ya kutosha na kuwa tayari kujaribiwa kabla ya kupokea ubatizo.

Mchungaji: Karibuni wapendwa kwa ajili ya kushiriki ibada ya sakramenti ya Ubatizo Mchungaji: Tukiwa katika hali ya kusimama tumwombe Mungu Wetu Mchungaji: Naomba kwa pamoja tukiri Imani ya Mitume inayotuunganisha na Wakristo wengine ulimwenguni kote; Mchungaji: Tukiwa katika hali ya kukaa, tuimbe wimbo namba……………. 11

Mchungaji: Tusikilize Neno la Mungu. (rejea 85-86) vifungu vya ubatizo) Baada ya kumalizika kwa sehemu ya kwanza: a) Mzee wa kanisa aliyevaa mavazi ya kizee atawaleta kwa mchungaji watu wanaopaswa kubatizwa b) Ikiwa ni watoto atawasogeza wazazi wao mbele (wazazi waandaliwe mapema zaidi wasimame na watoto wao c) Ikiwa ni ubatizo wa kunyunyiza, basi maji yaandaliwe mapema katika chombo maalum d) Ikiwa ni ubatizo wa kuzamisha basi dimbwi au sehemu ya kubatiziwa iandaliwe mapema; na ikiwa ni mbali na kanisa, basi sehemu ya kwanza ya ibada hii inaweza kufanyika kanisani

Mchungaji: Nitamkaribisha mzee…………… aweze kuwakabidhi wanaobatizwa leo Mzee: kwa niaba ya kanisa Ninawawasilisha/ninamwasilisha……(taja majina) kwa ajili ya kupokea sakramenti ya Ubatizo. Mchungaji: (akiwaelekea wanaopokea ubatizo/ wazazi wanaoleta watoto kwa ubatizo, au wasimamizi wengine) Ningependa 12

kuwauliza maswali ambayo ni sehemu ya viapo vyenu kwa Bwana. Kwa wakubwa (kila mmoja ajibu kibinafsi lakini kwa pamoja watajibu) Mchungaji: Je ni kweli unataka kupokea Sakramenti ya ubatizo? Watahiniwa: ndiyo ninataka Mchungaji: je unakubali kumkiri upya Yesu kuwa Bwana na Mwokozi wa maisha yako? Mtahiniwa: ndiyo ninakubali Mchungaji: Je unaahidi kwa neema ya Mungu kuendelea kuwa mshirika wa kanisa hili? Watahiniwa: Ndiyo ninaahidi Mchungaji: Je, utakuwa mwanafunzi mwaminifu wa Kristo, kutii Neno lake na kuonyesha upendo wake kwa wengine? Watahiniwa: ndiyo Kwa wazazi (ikiwa wanaobatizwa ni watoto) Mchungaji: je ni kweli unataka mtoto wako apokee Sakramenti ya Ubatizo? 13

Mzazi/mlezi: ndiyo ninataka Mchungaji: Je! Unaahidi kupitia sala na maisha yako ya mfano, kumsaidia mwanao na kumfundisha kuwa Mkristo mwaminifu mpaka atakapopokea uthibitisho? Mzazi/mlezi: ndiyo ninaahidi Kwa kanisa zima (watu wote wasimame) Mchungaji: Je, ninyi Washirika wote wa kanisa hili, kwa upendo mnakubali kuwaombea waumini hawa wapya, kuwatia moyo na kuwahimiza kumjua na kumfuata Kristo na kuwa washirika waaminifu wa kanisa lake? Wote: ndiyo tunakubali Mchungaji: Mnakubali kuwapokea katika ushirika huu wa ……(taja jina la kanisa) ili wawe washirika waaminifu, na kwamba waweze kutumia vipawa vya Roho Mtakatifu kwa ajili ya kuwaleta wengine kwa Yesu? Wote: ndiyo tunakubali Mchungaji: (akiwaelekea wanaobatizwa) ndugu zangu wapendwa katika Bwana; kwa kuwa 14

ninyi wenyewe mmekiri kwa kuwa na nia ya dhati ya kubatizwa, ningependa niwakumbushe maneno haya kwamba, mnapopokea ubatizo, mnaingia katika agano ambalo Mungu ameanzisha. Ndani ya agano hili Mungu hutupatia maisha mapya, hutulinda na maovu, na hutulea kwa upendo. Maelekezo: Ubatizo siyo suala la maji mengi wala maji machache, na pia siyo suala la watu wazima au watoto. Hivyo kama kanisa tunatambua ubatizo wa aina zote; maji mengi na machache, kuzamisha au kunyunyiza, watoto au watu wazima. Hili limeachwa kwa maamuzi ya makanisa. Amueni mapema aina ya ubatizo wenu na mzingatia mambo yafuatayo: -

a) kama ni ubatizo wa kuzamisha, basi ni lazima kuandaliwe nguo za kubadilisha kwa watakaobatizwa, au mavazi maalum. Ni muhimu kanisa kuamua mapema aina gani ya ubatizo litatumia. Mchungaji ataingia moja kwa moja majini na kuwaita mmoja kwa mwingine. b) kama wanaobatizwa ni watoto wachanga, basi wazazi watajipanga mbele ya mchungaji na mzee wa kanisa atasoma majina yao na kila mzazi atapeleka mtoto wake hapo mbele. 15

Mchungaji atachonya mkono wake bakulini na kuchota maji kidogo na kumimina kwenye paji la uso au kichwa cha mtoto;

c) kama ni maji machache, wanaobatizwa wanapaswa kupiga magoti mbele ya mchungaji. d) Wanaobatizwa watapatizwa mmoja mmoja hata kama wakiwa wengi.

Mchungaji: Tuombe kwa ajili ya kubariki maji (mchungaji aombe kwa maneno yake)

Mchungaji: Wewe…………. (taja jina) ninakubatiza kwa jina la Baba, na la Mwana na la Roho Mtakatifu Wote: Amina Mchungaji: (baada ya ubatizo) tuombe “Ee Bwana, mshikilie sasa mtoto wako kwa Roho wako Mtakatifu. Mpe roho ya hekima na ufahamu, roho ya ushauri na nguvu, roho ya maarifa na kumcha Bwana, roho ya furaha mbele yako, wakati wote, sasa na hata milele. Wote: Amina

16

Mchungaji: Ee Mwenyezi Mungu, mtetee mtumishi wako na uachilie neema yako ya mbinguni, ili aendelee kuishi kwako milele kanisa maisha haya na yale yajayo; na kila siku uzidi kumwongoza kwa Roho wako Mtakatifu, mpaka atakapokuja kwenye ufalme wako wa milele. Wote: Amina Mchungaji: Sasa wewe umetiwa muhuri na Roho Mtakatifu katika ubatizo, na kupandikizwa ndani ya Kristo milele. Mzee

wa kanisa: Kwa furaha na shukrani tunawakaribisha katika kanisa la Kristo kushiriki nasi katika huduma yake, kwa maana sisi sote tu moja katika Kristo. Sasa tunawapokea ninyi kama washirika kamili wa kanisa hili;

Wote: Amina Mchungaji: Ni wakati wa kupokea vyeti vya ubatizo Mchungaji: Sasa, pokeeni baraka za Mungu ninyi nyote mnaomtegemea Yeye, Neema ya Bwana Wetu Yesu Kristo, na Upendo wa 17

Mungu baba, ukae nanyi nyote, sasa na hata milele, Maelekezo: a) kama kuna mambo mengine yanayohusiana na ubatizo yataelekezwa na wazee wa kanisa. Hapa ndipo mwisho wa ibada.

b) Waliobatizwa wanapaswa kupewa maelekezo namna ya kushiriki meza ya Bwana. Ikiwezekana wafanye mazoezi ya kushiriki meza ya Bwana ili wasipate shida kushiriki kwa mara ya kwanza.

2. Ibada ya Meza ya Bwana Maelekezo: Kama ikiwezekana, ibada hii ifanyike kila mwezi angalau mara moja, kama mchungaji akiweza kufanya mara mbili kwa mwezi, ni baraka kwa kanisa hilo. Ni muhimu kuwaandaa Washiriki kujiandaa na meza ya Bwana kabla ya Juma moja. Mchungaji anaweza kupeleka Ibada ya Meza ya Bwana kwa wale ambao hawawezi kuja kanisani kwa sababu ya ugonjwa au uzee. Mchungaji anapaswa kuhakikisha kama mikate na vikombe vinatosha kwa ajili ya washirika wote. Kama havitakuwa vinatosha, basi anapaswa kung’amua mapema kwamba atafanyaje. 18

Mchungaji: Naomba wote tusimame na kuanza ibada ya Meza ya Bwana. Mchungaji: Tuanze ibada kwa jina la Mungu baba na Mwana na Roho Mtakatifu Wote: Amina Mchungaji: Tuimbe wimbo…………. Mchungaji: Tuombe (mchungaji ataomba maombi ya kufungua)

Mwenyezi Mungu tunakushukuru kwa ajili ya kumtuma Mwana wako Yesu Kristo kwa ajili ya kufanyika sadaka kwa ajili ya dhambi zetu. Tunaomba sasa ubariki tendo hili la kupokea mwili na damu ya Kristo kwa imani. Ninaomba kwa jina la YesuMchungaji: Tukae sote Mchungaji: Wapendwa katika Bwana, Bwana wetu Yesu Kristo katika usiku ule aliosalitiwa alianzisha Sakramenti hii ya Meza ya Bwana, ambayo ni Sakramenti ya mwili wake na damu. Sakrmenti hii inapaswa kuzingatiwa katika Kanisa lake hadi mwisho wa ulimwengu kwa ukumbusho wa milele 19

wa kujitolea kwake mwenyewe katika kifo chake msalabani. Meza ya Bwana inatukumbusha chakula cha kiroho na ukuaji wetu katika Kristo Yesu na hutusaidia pia katika kufanya majukumu tunayopaswa kufanya mbele za Mungu, vilevile inaonyesha uhusiano wetu wa karibu na Yesu. Wapendwa, katika sakramenti hii, Kristo hajatolewa kwa Baba yake kama dhabihu halisi, bali ni ukumbusho kwa kuwa aliyejitolea mwenyewe, peke yake, juu ya msalaba, mara moja kwa wote. Sadaka yake ndio kitu pekee kinachoweza kulipa dhambi zetu. Kwa hiyo tunapoenda kupokea sakramenti hii, tupaswa kupokea kwa imani. Mchungaji: Tuombe: “Asante Bwana wetu Yesu Kristo, kwa kuanzisha Sakramenti hii. Na sasa ninaweka wakfu mkate na divai kwa ajili ya matumizi maalum ya Meza ya Bwana. Ninaomba uwepo wako Kristo Kiroho ukashuke katika mkate na divai. Ninaomba katika jina la Yesu. Amina

20

Mchungaji: Tunapoenda kushiriki tendo hili takatifu, tukumbuke maneno ya Mungu kupitia mtume Paulo katika I Wakorintho 11:28 ‘lakini mtu ajihoji mwenyewe na hivyo aule mkate na kukinywea kikombe’ Hii inamaanisha kwamba mtu asiye na ufahamu wowote, au ikiwa ametenda dhambi, hapaswi, na wala haruhusiwi kushiriki Meza ya Bwana; kwani ni chukizo mbele za Mungu kushiriki katika siri hii takatifu ukiwa na mawaa. Kwa hiyo kila mmoja ajitafakari mwenyewe kabla ya kupokea mwili na damu, ili asije akala na kunywa kwa hukumu yake. Vilevile mtu yeyote ambaye bado hajapokea Sakramenti ya Ubatizo haruhusiwi kushiriki katika Meza ya Bwana; wala watoto hawaruhusiwi kushiriki Meza ya Bwana. Na hivyo inahitajika yeyote anayepokea Meza ya Bwana awe na ufahamu sahihi na kujitafakari mwenyewe. Maelekezo: Mchungaji atamwita mzee wa kanisa au yeyote anayemsaidia kwa ajili ya kufungua 21

kitambaa kilichofunika mkate na divai. Watafungua kwa utaratibu na kwa umakini na heshima mbele ya Meza ya Bwana, kwani ni tendo takatifu sana mbele za Mungu

Mchungaji: (akiwa ameinua mkate) Bwana Yesu usiku ule aliotolewa aliutwaa mkate, naye akiisha kushukuru akaumega akasema ‘huu ndio mwili wangu ulio kwa ajili yenu, fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu. Maelekezo: Atampa mzee/shemasi au mtu yeyote aliyeandaliwa kwa ajili ya kugawa mkate kwa watu wote wanaoshiriki; kabla ya kumpa, mchungaji anapaswa kuchukua kwanza yeye mkate na baadaye kukabidhi kwa mzee wa kanisa ili agawe kwa washirika wengine. Baada ya kugawa, mzee wa kanisa anapaswa kumkabidhi mchungaji chombo cha mkate, na kisha mchungaji atamkabidhi mzee wa kanisa mkate. Itakuwa vivyo hivyo hata kwa kikombe. Wakati wa kugawa mkate nyimbo za vitabuni vinavyohusu mateso ya Kristo zinaweza kuimbwa kwa sauti ya chini ili kuruhusu watu kutafakari ukuu wa Mungu. Ala za muziki pia zinaweza kutumika. 22

Mchungaji: Nawasihi ndugu zangu mnaopokea, mpokee kwa unyenyekevu mbele za Mungu (awaelekeze watu kuchukua kila mtu mkate) kama tumekwisha kupokea wote na tule sote! Mchungaji: (huku akiinua kikombe) vivi hivi baada ya kula akakitwaa kikombe akasema “kikombe hiki ni agano jipya katika damu yangu, fanyeni hivi kila mnywapo kwa ukumbusho wangu.” Mchungaji: (hakikisha kila mmoja amekwisha kupata kikombe) na tunywe sote. Mchungaji: Kila mmoja amshukuru Mungu kwa ajili ya kazi yake kubwa ya wokovu katika maisha yako. Omba Mungu akutie nguvu katika maisha yako; na uendelee kupokea neema kupitia Neno la Mungu na Sakramenti tuliyoshiriki. Mchungaji: Tuimbe wimbo………. Mchungaji: Mwenyeji Mungu asante kwa ajili upendo wako mkuu kwa kumtuma Yesu Kristo ili kukamilisha kazi ya wokovu katika maisha yetu. Sisi watoto wako, kupitia Sakramenti ya meza ya Bwana tumepokea neema 23

zaidi na zaidi na ushirika wetu pamoja nawe umeimarika. Tunaendelea kuja mbele zako sasa tunaomba ushirika huu uendelee zaidi na zaidi mpaka Yesu atakaporudi tena. Tunaomba katika jina la Yesu Mchungaji; Na sasa, “Neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, na upendo wa Mungu baba, na ushirika wa Roho Mtakatifu, ukae nanyi nyote, sasa na hata milele.

24

III. IBADA ZA MAOMBI Kuna aina mbalimbali za ibada za maombi na maombezi, ambapo si rahisi kuzitaja zote katika kitabu hiki. Ukiachilia kwamba kanisa linapaswa kuomba kila siku, kuna ibada ambazo makanisa yote yanapaswa kuzingatia. Ibada hizo katika kanisa letu ni hizi zifuatazo:

1. Ibada ya Maombi ya Ki-Danieli i.

Haya ni maombi maalum ya kitaifa kwa kila mwaka ambayo yatafanyika mara mbili kwa mwaka; • yataanza kila Jumamosi ya Juma la tatu la mwezi wa tatu (3) • kwa mara ya pili yatafanyika kuanzia Jumamosi ya juma la tatu la mwezi wa kumi na moja (11) ii. Maombi haya ni kwa muda wa majuma matatu kamili (yaani siku 21) (Danieli 10:2). Waombaji wataanza kuhesabu kuanzia Jumamosi tajwa hapo juu, na kumaliza baada ya majuma matatu kamili. iii. Ni maombi ya kuomba toba maalum kwa ajili ya kanisa, nchi, familia. Ni maombi ya kuomboleza mbele za Bwana. 25

iv.

v. vi.

vii.

viii.

ix.

Katika maombi haya wakristo wanaweza kuamua kufunga au kutokufunga kwa kutegemeana na utaratibu wa kanisa husika. Washirika watapaswa kuhudhuria kanisani na kuomba pamoja. Muda wa maombi haya utategemea eneo husika; inawezekana ikawa asubuhi au jioni Katika maombi haya, maombezi binafsi yatakuwepo; kwamba kila mtu anaweza kupeleka mahitaji yake ya kuombewa. Katika maombi haya, inashauriwa kuandaa sadaka kila siku (ingawa siyo lazima lakini muda wa kutoa sadaka utakuwepo) Katika maombi haya, watu wanaruhusiwa kuweka nadhiri zao kwa Mungu kwa ajili ya mambo maalum ya kuombea. Mwishoni mwa ibada watu wapewe muda wa kutosha kuomba, na wale ambao watapenda kuendelea na maombi wasizuiwe.

2. Ibada ya Maombi ya Jumatano Kila Jumatano kutakuwepo na ibada ya maombi kwa kanisa zima. Kwa hivyo washirika wote wanapaswa kuhudhuria katika maombi haya: i. Kanisa la mahali linaweza maombezi maalum. 26

kuwa

na

ii. Wakristo wataruhusiwa kutaja maombezi mengine ambayo wanaona ni muhimu kushirikisha wengine. iii. Kiongozi anapaswa kuhakikisha kwamba anawapa watu muda wa kutosha kumwomba Mungu. iv. Kanisa la mahali linaweza kuamua ni muda gani maombi haya yafanyike kwa kuzingatia eneo husika.

3. Ibada ya Maombi ya Ijumaa i. ii.

iii. iv.

v.

Haya ni maombi maalum kwa ajili ya wanawake. Viongozi wa wanawake watawajibika kupanga muda wa kukusanyika kwa kuzingatia eneo husika. Yanaweza kufanyika kanisani, au sehemu yoyote ile ambayo wanawake watakubaliana. Kiongozi wa ibada hii anaweza kuwa mama mchungaji, mama mwinjilisti, mzee au shemasi wa kike, mwenyekiti wa wanawake, au mwanamke mwingine yeyote ambaye ni Mkristo mkomavu. Kutakuwepo na matoleo katika ibada ambayo yatalenga kuboresha idara ya wanawake.

27

4.

Ibada ya Maombi ya Idara

Kila idara ndani ya kanisa itakuwa na siku yake ya maombi. i.

ii.

iii.

Idara ya vijana inaweza kupanga maombi kati ya siku zifuatazo; Jumanne, Alhamisi, Jumamosi. Idara ya wababa inaweza kupanga maombi kati ya Jumatatu na Jumamosi au hata Jumapili jioni kama siku hiyo haitakuwa na ibada nyingine. Idara zingine ambazo hazijatajwa hapa zinaweza kupanga ibada katika siku yoyote kwa muda ambao hautaingiliana na ibada zingine.

5. Ibada ya Maombi ya Kifamilia i. Kila familia inapaswa kuwa na ibada ya maombi kila siku. ii. Inawezekana ikafanyika asubuhi na jioni, lakini ni muhimu ifanyike angalau mara moja kwa siku. iii. Kila familia itaamua muda. iv. Kipindi cha neno kila familia wanaweza kuamua kutumia kwa kusoma neno la Mungu kwa pamoja na kushiriki maombi. 28

v. Kama familia pia wanaweza kuanzisha usomaji wa Biblia kuanzia kitabu cha Mwanzo mpaka Ufunuo.

Taratibu za ibada za Maombi Maelekezo: Ibada za maombi zitakuwa na viongozi wa aina mbili; kiongozi wa ibada na mhubiri tu. Utaratibu wa ibada za maombi utakuwa na mtiririko ufuatao: 1. Kuanza ibada kwa nyimbo za tenzi/sifa nk. 2. Kukiri imani ya mitume. 3. Kusifu na kuabudu au nyimbo za vitabuni. 4. Kusikiliza Neno la Mungu. 5. Kutaja maombezi. 6. Maombi na maombezi kwa pamoja (ni vizuri kuomba kwa pamoja, na mwisho mtu mmoja anaweza kumalizia maombi hayo) 7. Matoleo (kwa kutegemeana na ibada). 8. Kusikiliza Matangazo. 9. Kufunga ibada kwa sala ya Bwana.

29

IV. IBADA ZA KISHEREHE Ibada za kisherehe ni zile ambazo zinakuwa haziko kwenye ratiba maalum ya kanisa (Yaani zinatokea mara chache tu).

1. Ibada ya Ndoa Maelekezo: Ibada ya ndoa inaweza kufanywa siku yoyote ile kwa kutegemea wale wanaofunga ndoa kwa nafasi zao. Suala la ndoa linajumuisha vipengele 3 muhimu sana ambavyo hutegemeana kila kimoja, vipengele hivyo ni; kanisa, serikali, na utamaduni. Kwa hiyo mchungaji kabla hajaamua kufungisha ndoa hiyo lazima ahakikishe kwamba vipengele vyote vimetekelezwa kwa jinsi inavyopaswa. Mchungaji husimama akiwakilisha kanisa na serikali pia.

Kiongozi: Ndugu zangu wapendwa, karibuni katika ibada ya ndoa kati ya…………….na………………kwa sasa ningependa kuwakaribisha wazazi wa pande zote mbili waingie. (wazazi wa Bwana arusi watakaa mkono wa kulia kwao, na kinyume chake)

30

Kiongozi: Karibuni bwana arusi na rafiki yako muingie. (wataingia kwa kutumia mlango wa mchungaji na wakifika mbele wasikae bali waendelee kusimama)

Kiongozi: Naomba bibi arusi na msafara wake waingie (watu wote wakiwa amesimama-wakifika katikati mwambie bwana arusi akutane na bibi arusi) Kiongozi: Bwana arusi kutana na bibi arusi na mweze kusogea mbele kwa pamoja (wakutane na akifika afunue shela kichwani, na baadaye waelekee katika maeneo yao ya kukaa)

Kiongozi: Nitakaribisha kwaya………….. Kiongozi: Basi, namkaribisha mchungaji ambaye anasimama kwa niaba ya msajili wa ndoa aweze kufunga ndoa hii. Mchungaji: Basi nawasihi watu wote tusimame na tuweze kukiri Imani ya Mitume inayotuunganisha na Wakristo wengine ulimwengu. Mchungaji: Nawasihi watu wote tukae Mchungaji: wapendwa, tumekusanyika hapa machoni pa Mungu na mbele za mkutano huu, ili 31

tuwaunganishe……… na ………...katiaka ndoa takatifu; ambayo ndiyo iliyo hali ya heshima, iliyoamriwa na Mungu, ikimpa mfano wa kuungamana kwa Kristo na kanisa lake. Hali hiyo takatifu Kristo aliiheshimu kwa kuwako yeye mwenyewe katika harusi ya Kana ya Galilaya kama ilivyoandikw katika Yohana 2:1-11. Kwa sababu hii basi watu wasiingie kwenye ndoa bila kufikiri, wala kwa kuingia kwa haraka, bali wanapaswa kuingia kwa heshima na kwa busara, na kwa makini na kwa kumcha Mungu. Kwa kuzingatia uzito na umuhimu wa ndoa, basi ningependa kuuliza miongoni mwenu kama kuna mtu ambaye ana sababu za msingi za kuzuia hawa ndugu wasiunganishwe kuwa mume na mke aseme sasa (tulia na kuangalia miongoni mwa mkutano. Kama kuna pingamizi sitisha shughuli)1

1

Mapingamizi ambayo tunaweza kuyapokea ni: a) Ikiwa anayeingia kwenye ndoa alikuwa na ndoa nyingine halali (yaani kuwepo na ushahidi wa cheti cha ndoa halali cha kiserikali. Mchungaji usijaribu kupokea mapingamizi ya wachumba. Kama mtu asipoweka Ushahidi wa kimaandishi, basi ndoa itaendelea kufungwa siku hiyo hiyo; b) Ikiwa kuna uthibitisho kwamba wanaofunga ndoa si mwanamke na mwanamume. Ndoa za jinsia moja ni mwiko kwetu. Kama ukithibitisha hakuna majadiliano zaidi ya kuahirisha ndoa hiyo;

32

Mchungaji: kwa kuwa hakuna sababu iliyotolewa kuzuia watu hawa wasifunge ndoa yao, sasa napenda kuuliza, ni nani anayemtoa ………...aolewe na…………? Mchungaji: (atawaambia wale wanaooana) nawaonya na kuwataka ninyi wawili, kama mtakavyojibu siku ya kutisha ya hukumu, siri za mioyo yote zitakapofunuliwa, baada ya kufikiria agano mnalotaka kulifanya mbele za Mungu na mbele za umati huu. Nawaulizeni ninyi sasa, je kuna mmojawapo kati yenu anajua wazi kabisa kwamba ana sababu zinazomzuia asifunge ndoa hii? Kumbukeni kwamba mnachoenda kukifanya mbele za Mungu ni kitendo kitakatifu, hivyo lazima kiingiwe katika hali ya ukweli na kicho mbele zake. Maharusi: (watajibu watakavyoona bora lakini kwa kawaida huwa hakuna sababu) hatuna sababu ya kutuzuia kufunga ndoa Mchungaji: Kwa kuwa sasa hakuna sababu yoyote inayowazuia kufunga ndoa, sasa nawaomba mwangaliane kila mtu na c)

Ikiwa kuna zuio la mzazi mmojawapo;

33

mwenzake ili niweze kuwafungisha ndoa yenu sawasawa na maneno ya Mungu. Maharusi: (waangaliane) Mchungaji: Ni vizuri sasa kupata kibali kutoka kwa wazazi wa jamaa hawa kwa ajili ya kufunga ndoa (anza kwa kuita upande wa kike na baadaye kiumeni) Mzazi: Mimi………. namtoa………. aolewe/amuoe ……. nakubali kutoka moyoni mwangu. Mungu awasaidie. Mchungaji: (atamwambia mwanaume kwa kutaja jina lake). …...utamtwaa …………. kuwa mke wako wa ndoa, muishi pamoja katika ndoa takatifu? Utampenda, utamfariji, utamheshimu, utamtunza, katika ugonjwa na katika afya na kuwaacha wengine wote na kushikamana naye katika maisha yako yote? Bwana harusi: Ndiyo ninakubali Mchungaji: (atamwambia mwanamke kwa kutaja jina lake) …...utamtwaa …………. kuwa mume wako wa ndoa, muishi pamoja 34

katika ndoa takatifu? Utampenda, utamfariji, utamheshimu, utamtunza, katika ugonjwa na katika afya na kuwaacha wengine wote na kushikamana katika maisha yako yote? Bibi harusi: Ndiyo ninakubali Mchungaji:(Maharusi

waangaliane na washikane mikono kwa ajili ya viapo vyao. kisha kila mmoja atafuatisha maneno ya mchungaji)

Nawasihi mshikane mikono sasa. Bwana harusi: Mimi __nakutwaa wewe__kuwa mke wangu wa ndoa tangu leo. Nitakuwa nawe katika mema na katika mabaya, katika utajiri na katika umaskini, katika ugonjwa na katika uzima, nitakupenda na kukutunza mpaka kufa, kwa amri takatifu ya Mungu; na kwa hiyo nakupa kiapo changu. Ee Mwenyezi Mungu nisaidie. Watu wote: amina! Bibi harusi: Mimi…………………na kutwaa wewe…………………. kuwa mume wangu wa ndoa tangu leo. Nitakuwa pamoja nawe katika mema na katika mabaya, katika utajiri na katika umaskini, katika 35

ugonjwa na katika uzima, nitakupenda na kukutunza mpaka kufa, kwa amri takatifu ya Mungu; na kwa hiyo nakupa kiapo changu. Ee Mwenyezi Mungu nisaidie. Mchungaji: Kwa kuwa ninyi nyote mmefanya maagano mbele za Mungu, je mna kitu gani kwa ajili ya kudhihirisha agano lenu? Bwana &Bi harusi: (watasaidiwa na wasaidizi wao kwa kutoa peke na kumpa mchungaji). Tuna pete hizi hapa! Mchungaji: Pete ya harusi ni ishara ya nje ionyeshayo ishara ya ndani na neema takatifu, inayoonesha umoja wote wa maharusi hawa. Pete haina mwanzo wala haina mwisho. Kwa hiyo upendo wenu usiwe na mwisho kama pete hizi. Bwana harusi: (atwae mkono wa kushoto wa bibi harusi kisha aseme) Nakuvalisha pete hii kuwa ushahidi wa nadhiri yangu kwako na kwamba nitashika yale niliyoahidi kwako. Bibi

harusi: (atwae mkono wa kushoto) Ninakuvalisha pete hii kuwa ushahidi wa 36

nadhiri yangu kwako, na kama ishara ya upendo wangu kwako usio na mwisho. Na kwamba nitashika yale niliyoahidi kwako. Mchungaji: (maharusi wakiwa wameshikana mikono atamwambia bwana harusi) kwa kuwa…………...na …………. Wamekubaliana pamoja kuingia katika ndoa takatifu na kushuhudia mbele za Mungu na umati huu, na wameahidi imani ya kila mmoja kwa mwenziwe, na kuitangaza kwa kushikana mikono na kwa kupeana pete, na sasa Mungu awalinde katika ndoa hii takatifu. Mchungaji (Atoe tamko) kwa kuwa bwana……....na bibi…… wameunganishwa katika ndoa takatifu ya Kikristo, kwa mamlaka niliyopewa na serikali kama msajili wa ndoa na kwa Mamlaka niliyopewa na dhehebu langu, kama mhudumu wa Injili, ninatangaza kwamba sasa hawa ni mume na mke. Mchungaji: (Wapige magoti mbele) Eee Mungu, Muumba na mhifadhi wa watu wote, tunaomba Baraka kwako kwa ndoa ya watumishi wako hawa! Wajaalie neema 37

ya kuishi maisha matakatifu mbele zako na kwa kushika sheria zako. Waepushe na balaa na majanga katika maisha yao. Nyumba yao iwe sehemu ya furaha na amani. Kwa Jina la Yesu Kristo. Mchungaji: (Awaambie waumini wote). Enyi wapendwa katika Bwana nawasihi kwamba waombeeni wapendwa hawa ili waishi maisha matakatifu yanayompendeza Mungu. Watieni moyo ili wafurahie maisha ya ndoa. Mchungaji: Huu ni wakati mzuri sasa tumtolee Mungu matoleo ya shukrani kwa ajili ya ndoa hii. Vilevile wakati huu maharusi watasaini vyeti vya ndoa. Mchungaji: Sasa nawakabidi vyeti vya kiserikali kama ushahidi wenu kila mmoja cheti chake (waonyeshe mbele ya umati). Mchungaji: Sisi kama kanisa la………...tunawapa vyeti vya kanisa kwa kutambua kwamba ndoa hii ni ndoa takatifu katika kanisa hili. Mchungaji: (Mchungaji omba baraka kwa ajili ya watu) na sasa neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, na Upendo wa Mungu baba, 38

na ushirika Mtakatifu, ukae nanyi nyote sasa na hata milele. Mchungaji: Kama kuna mtu ana matangazo kwa ajili ya utaratibu unaoendelea sasa. Maelekezo: baada ya hapo ibada itakuwa imefikia mwisho na taratibu za kikanisa zitakuwa zimeishia hapo. Kiongozi: (sasa unaweza kuendelea na taratibu zingine, mchungaji amemaliza kazi yake na wala hahusiki na masuala ya ukumbini).

2. Ibada ya Mazishi Maelekezo: Inapendekezwa kwamba ibada ya mazishi isifanyike Jumapili labda kama imelazimu sana. Ibada hii inaweza kufanywa katika sehemu tatu; nyumbani, kanisani na makaburini. Hivyo basi kiongozi wa ibada hii lazima awasiliane mapema na wahusika wa msiba kabla kuandaa shughuli ya mazishi.

Kiongozi: Tuanze ibada ya mazishi kwa jina la Mungu Baba, na Mwana na Roho Mtakatifu. Wote: Amina. 39

Kingozi: Tuombe (kiongozi wa ibada aombe). Kiongozi: Sasa tusikilize wimbo wa faraja kutoka kwa waimbaji. Kiongozi: Sasa hivi tusikilize historia ya marehemu (ndugu aliyeandaliwa asome historia hiyo). Kiongozi: Wakati huu tusikilize neno la Mungu kutoka kwa……….. (vifungu vya kuhubiri rejea uk. 87).

Kiongozi: Tuombe (kiongozi anaweza kuomba yeye au mtu mwingine aliyechaguliwa). Kiongozi: Sasa tusikilize matangazo kutoka kwa mtu aliyeandaliwa. (matangazo haya yanahusu pengine ni wapi wanaenda kuzika au kama wanasafirisha, lazima watu walioko hapo wajulishwe mapema).

Kiongozi: Sasa ni wakati wa kutoa heshima zetu za mwisho kwa marehemu. (wakati wa kuaga ni vizuri kutumika kwa ajili ya kutoa sadaka pia). Ibada makaburini Maelekezo: Baada ya kufika kaburini watu wazunguke kaburi na kisha jeneza lishushwe kaburini 40

kwa taratibu kwa kuzingatia watu ambao wameandaliwa.

Kiongozi: kwa jina la Mungu Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu. Wote: Amina. Kiongozi: Ndugu zangu wapendwa sikilizeni neno la Mungu lisemavyo katika Maandiko Matakatifu; Warumi 14:8 “Kwa maana kama tukiishi, twaishi kwa Bwana, au kama tukifa, twafa kwa Bwana. Basi kama tukiishi au kama tukifa, tu mali ya Bwana.” I Wakorinto 15:21-23 “Maana kwa kuwa mauti ililetwa na mtu, kadhalika na kiyama ya wafu ililetwa na mtu. Kwa kuwa kama katika Adamu wote wanakufa, kadhalika na katika Kristo wote watahuishwa. Lakini kila mmoja mahali pake; limbuko ni Kristo; baadaye walio wake Kristo, atakapokuja.” Ufunuo 14:13 41

“Nikasikia sauti kutoka mbinguni ikisema, Andika, Heri wafu wafao katika Bwana tangu sasa. Naam, asema Roho, wapate kupumzika baada ya taabu zao; kwa kuwa matendo yao yafuatana nao.” Ayubu 14:1,2,5 “Mwanadamu aliyezaliwa na mwanamke Siku zake za kuishi si nyingi, naye hujaa taabu. Yeye huchanua kama vile ua, kisha hukatwa; Hukimbia kama kivuli, wala hakai kamwe.” Kiongozi: Tusikilize neno la Mungu kupitia Mtumishi……… (yasizidi dakika 5 tu) (kiongozi ashike udongo katika mkono wake wa kulia na aseme maneno haya).

Kiongozi: Mungu amemwita ndugu yetu……...kwa hiyo tunauweka mwili wake kaburini ili airudie ile ardhi (atupe udongo kaburini) kwa maana u mavumbi, (atupe udongo tena) na mavumbini utarudi (atupe udongo tena). Ndugu zangu tunapaswa kujua kwamba ndugu yetu atafufuliwa siku ya mwisho, 42

kama yasemavyo Maandiko. Lakini tukumbuke pia kwamba ingawa amekufa, kifo hiki ni kwa upendo wa Mungu, kwa ajili ya kumweka huru kabisa kutoka kwenye dhambi na taabu na kumfanya awe na uwezo wa ushirika zaidi na Kristo katika utukufu. Kwa wale ambao tunayo matumaini ya kumwona tena tunao ujasiri wa kusema kwamba “kwa heri ndugu yetu duniani” Amina. Kiongozi: Ni wakati wa kuweka udongo ndani ya kaburi (watu muhimu kama vile ndugu, marafiki, au majirani wanaweza kupangwa maalum)

wa kwa

marehemu utaratibu

Kiongozi: Anzeni kufukia sasa (watu wafukie kaburi huku nyimbo za tenzi za rohoni zikiimbwa na wapendwa wengine. Nyimbo zifuatazo zinaweza kuimbwa hapo: Na. 9, 50, 58,101,102 na 103.) Kiongozi: Sasa ni wakati wa kuweka mashada ya maua ambayo ni ishara ya upendo (mashada yawe matano tu na la sita ataliweka kiongozi wa ibada ambalo ni shada la msalaba. Kama kuna watu wengine walio na 43

mashada na kama wameandaliwa basi waruhusiwe kuyaweka kwa utaratibu mzuri)

Kiongozi: Ni wakati wa shukrani. (kwa upande wa familia na kwa upande wa kanisa kwaa kuwashukuru ambao wameshiriki mazishi). Kiongozi: Tuombe kwa kuhitimisha ibada hii. Kiongozi (kama kiongozi akiwa ni mchungaji atatoa baraka). Kiongozi; Huu ndio mwisho wa ibada hii. Kwa herini! Tangazo Muhimu: Kwa kuwa sisi ni Wakristo, ibada yetu imeishia hapa, kanisa halihusiki na mambo ya mila na tamaduni zingine. Kiongozi: Kwa washirika wote wa kanisa letu, tunaomba tukutane katika familia ya marehemu kwa ajili ya faraja zaidi. Maelekezo: kama kanisa mnaweza kupanga watu kadhaa kila siku angalau kwa siku tatu mfululizo kwa ajili ya kufanya ibada fupi asubuhi na jioni.

44

3. Ibada ya Kusimika Wachungaji Kiongozi: Naomba msafara wa Wachungaji, waleseni na Wainjilisti waingie ndani ya kanisa sasa ili tuanze ibada yetu. Wakati huo tutakuwa tunaimba wimbo………… Kiongozi: Watu wote tusimame ili tuanze ibada yetu. Kiongozi: Kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu. Kiongozi: Tuombe sala ya Kimya (kama dakika moja hivi, baada ya sala ya kimya kiongozi ataomba kwa sauti kubwa).

Kiongozi: Basi nawasihi watu wote tusimame na tuweze kukiri Imani ya Mitume inayotuunganisha na Wakristo wengine ulimwengu. Kiongozi: Nawasihi tukae sote na tuimbe wimbo wa namba. Kiongozi: Nimkaribishe Mchungaji ………aongoze maombi.

45

Kiongozi: Ningependa zifuatazo

kukaribisha

kwaya

Kiongozi: Niwaombe sote tusimame kwa ajili ya kumwabudu Mungu kwa wimbo (kiongozi anaweza akaangalia mazingira kama yanakubalika). Kiongozi: Sasa tutasikiliza neno la Mungu kutoka kwa………… Kiongozi: Huu ni wakati wa kutoa matoleo mbele za Mungu. (kwaya inaweza kuimba au wimbo wa kitabuni) Kiongozi: Sasa nimkaribishe Modereta kwa ajili ya kazi ya kusimika wachungaji Modereta: Namkaribisha Mchungaji……. ambaye ni Katibu wa kamati ya Usimikaji awaite majina waleseni ambao leo wataenda kusimikwa kuwa wachungaji. Kila atakayeitwa atasimama mbele. Modereta: Ni wakati wa kujibu maswali; 1. Je unamwamini Mungu baba, Mwana na Roho Mtakatifu, nawe unakubali kumkiri upya Bwana Yesu Kristo kuwa Bwana na Mwokozi wa Maisha yako? 2. Je unakubali neno la Mungu lililo katika Maandiko ya Agano la Kale na Agano 46

Jipya kwamba ndiyo msingi mkuu wa mafundisho ya kanisa hili? 3. Je kwa moyo mkamilifu unakubali kupokea kiri zote za Imani zinazofundishwa na kanisa hili? 4. Je unakubali kwamba muundo wa utawala wa kanisa hili unaafikiana na neno la Mungu? 5. Je unaahidi kutafuta umoja na Amani ya kanisa hili, kuyainua mafundisho yake, ibada, uongozi, nidhamu na kuhifadhi moyo wa udugu kwa wafuasi wote wa Bwana? 6. Je unakubali kutii katiba na kanuni za kanisa hili zilizopitishwa na Mkutano Mkuu na kwamba utashirikiana na uongozi katika utekelezaji wake?

Modereta: Kwa kuwa wote mmekubali kutumika katika shamba la Bwana sawasawa na mwito wenu, sasa basi Pigeni Magoti mbele za Mungu na mbele za Kanisa, na ninawaomba wachungaji wote muweke mikono juu yao. Maelekezo: wazee wa kanisa hawapaswi kuweka mikono juu ya wachungaji Modereta: Huu ni wakati wa kuvishwa majoho na kora. Maelekezo: kila mleseni kabla ya kuanza ibada atachagua mchungaji atakayemvika joho 47

lake-na hivyo mchungaji huyo atakuwa tayari ili kuzuia mkanganyiko. Modereta: Kwa mamlaka niliyopewa na dhehebu la Kipresbiteri, ninatangaza kwamba ninyi ni wachungaji kamili; Kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu-Amina. Kiongozi: Sasa nitamkaribisha……… ili awakabidhi vyeti vya usimikwa. Kiongozi: Sasa tutakabidhi alama za kanisa kwa kila mchungaji, tayari kwa ajili ya kuendelea na huduma rasmi katika kanisa hili. Maelekezo: Alama za kanisa ni neno (Biblia) na Sakramenti (vyombo vya Meza ya Bwana) kama ishara ya kanisa letu. (vifaa hivi viandaliwe mapema, na atakabidhiwa mchungaji husika. Wachungaji watakaosimikwa ndio wanawajibika kuandaa vyombo hivi mapema iwezekanavyo.

Kiongozi: Sasa nitakakaribisha watu wafuatao kwa ajili ya kutoa pongezi zao. Kiongozi: Nitamkaribisha mchungaji…… kwa ajili ya kusoma Matangazo. Kiongozi: Nawaomba tusimame tuimbe wimbo namba………. beti moja na korasi yake. 48

Kiongozi: Sasa nitamkaribisha Mchungaji……...kwa ajili ya kutoa baraka. Kiongozi: Tutoke nje kwa utaratibu maalum.

4. Ibada ya Kusimika Wazee wa Kanisa Maelekezo: Wazee wa kanisa watasimikwa katika makanisa yao wanayotumika, na kwamba uzee wao hauhamishwi kwa kanisa lingine isipokuwa watapitia michakato ileile ya kupatikana. Vilevile ni mchungaji peke yake mwenye mamlaka ya kusimika mzee.

Kiongozi: Naomba watu wote tusimame, na sasa naomba msafara wa wazee wa kanisa waingie ndani ya kanisa sasa ili tuanze ibada yetu. Wakati huo tutakuwa tunaimba wimbo…… Kiongozi: Kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu Kiongozi: Tuombe sala ya Kimya (kama dakika moja hivi, baada ya sala ya kimya kiongozi ataomba kwa sauti kubwa)

49

Kiongozi: Basi nawasihi watu wote tusimame na tuweze kukiri Imani ya Mitume inayotuunganisha na Wakristo wengine ulimwengu. Kiongozi: Nawasihi tukae sote na tuimbe wimbo wa namba…… Kiongozi: Nimkaribishe Mch.…………aongoze maombi. Kiongozi: Ningependa kukaribisha kwaya zifuatazo……….. Kiongozi: Niwaombe sote tusimame kwa ajili ya kumwabudu Mungu kwa wimbo (kiongozi anaweza akaangalia mazingira kama yanakubalika). Kiongozi: Sasa tutasikiliza neno la Mungu kutoka kwa…………… Kiongozi: Ni wakati wa kutoa matoleo mbele za Mungu. (kwaya inaweza kuimba au wimbo wa kitabuni). Kiongozi: Huu ni wakati wa kusimika wazee wa kanisa (kabla ya kuanza, kiongozi lazima ahakikishe kwamba wazee wanayo majoho yao kila mmoja). 50

Mchungaji: Naomba sasa wazee wa kanisa simame mbele za Mungu. Mchungaji: Sasa nitawauliza maswali naomba mujibu kwa kadri inavyotakiwa 1) Je unamwamini Mungu baba, Mwana na Roho Mtakatifu, nawe unakubali kumkiri upya Bwana Yesu Kristo kuwa Bwana na Mwokozi wa Maisha yako? 2) Je unakubali neno la Mungu lililo katika Maandiko ya Agano la Kale na Agano Jipya kwamba ndiyo msingi mkuu wa mafundisho ya kanisa hili? 3) Je unakubali kutii katiba na kanuni za kanisa hili zilizopitishwa na Mkutano Mkuu na kwamba utashirikiana na uongozi katika utekelezaji wake?

Mchungaji: Kwa kuwa wote umekubali kutumika katika shamba la Bwana sawasawa na wito wako, sasa basi piga magoti mbele za Mungu na mbele za Kanisa, na ninawaomba wachungaji wote na wale wamisionari wachungaji msimame nyuma ya wazee/mzee hawa kwa ajili ya kuweka mikono juu yao kwa kuwasimika rasmi. Maelekezo: wakati huo wachungaji wote wataweka mikono yao juu ya wazee na kuomba kwa pamoja. Wazee wa kanisa ambao 51

walishasimikwa hawawezi kuweka mikono juu ya wazee wenzao. Ni wachungaji peke yao.

Modereta: Huu ni wakati wa kuvishwa majoho. (mchungaji kiongozi atawavika majoho)

Modereta: Kwa mamlaka niliyopewa na dhehebu la langu la Kipresbiteri, ninatangaza rasmi kwamba kwamba hawa ni wazee wa kanisa hili la…… Kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu-Amina. Kiongozi: Sasa nitamkaribisha…… ili awakabidhi vyeti vya usimikwa. Kiongozi: Sasa nitakakaribisha watu wafuatao kwa ajili ya kutoa pongezi zao: Kiongozi: Nikaribishe mzee mwakilishi kwa ajili ya Neno la Shukrani. Kiongozi: Nitamkaribisha mchungaji……….. kwa ajili ya kusoma Matangazo Kiongozi: Nawaomba tusimame na tuimbe wimbo namba........ Kiongozi: Sasa nitamkaribisha Mchungaji ……. kwa ajili ya kutoa Baraka. Kiongozi: Tutoke nje kwa utaratibu maalum.

52

5. Ibada ya Kuingiza Watumishi Kazini Maelekezo: Watumishi ambao wanaweza kuingizwa kazini ni pamoja na mashemasi, viongozi wa idara na viongozi wengine wa kitaifa.

Kiongozi: Naomba watu wote tuingie ndani ya kanisa kwa ajili ya kuanza ibada yetu. Kiongozi: Watu wote tusimame ili tuanze ibada yetu. Kiongozi: Kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu. Kiongozi: Tuombe sala ya Kimya. Kiongozi: Basi nawasihi watu wote tusimame na tuweze kukiri Imani ya Mitume inayotuunganisha na Wakristo wengine ulimwengu. Kiongozi: Nawasihi tukae sote na tuimbe wimbo wa namba……… Kiongozi: Nimkaribishe Mchungaji…… aongoze maombi. Kiongozi: Ningependa kukaribisha kwaya zifuatazo. 53

Kiongozi: Sasa tutasikiliza neno la Mungu kutoka kwa…………… Kiongozi: Sasa nitamkaribisha………………. aweze kuwaingiza kazini viongozi wafuatao katika nafasi za utumishi. (taja majina yao)

Mchungaji: Ndugu zangu mnaoingizwa kazini leo, simameni na nitawauliza maswali. 1. Je mnakubali kutii katiba na mwongozo wa wa kanisa hili kama ulivyopitishwa na Mkutano Mkuu? 2. Je mnakubali kufanya kazi zenu zote kwa ushirikiano na wengine?

Mchungaji: Kwa kuwa mmekubali, basi pigeni magoti mbele za Mungu, na tutaomba pamoja kwa ajili ya kuwakabidhi katika mikono salama ya Mungu wetu. Maelekezo: watu wote wote wataomba. Wachungaji watainuia juu mikono yao kuelekea kwa wale ambao wanaingizwa kazini.

Kiongozi: Nimkaribishe………. kwa ajili ya kutoa vyeti kwa wanaoingia kazini. Kiongozi: Nimkaribishe …………kuwakabidhi vyeti wastaafu. 54

Maelekezo: kama kuna watu wanataka kupiga picha kwa pamoja, tafadhali kiongozi unapaswa kutoa maelekezo haraka.

Kiongozi: Nikaribishe watu wafuatao kwa ajili ya pongezi na nasaha. Kiongozi: Huu ni wakati wa kutoa Sadaka…. kwaya itaimba. Modereta: Wakati huu ningependa kumkaribisha… kwa ajili ya neno la shukrani. Kiongozi: tusikilize matangazo ya leo Kiongozi: tusimame tuimbe wimbo wa namba…… Kiongozi: Nimkaribishe mchungaji…………. kwa ajili ya kuomba baraka.

6. Ibada ya Kutoa kibali cha kuhubiri

(Leseni) Kiongozi: Naomba watu wote tuingie ndani ya kanisa kwa ajili ya kuanza ibada yetu. Kiongozi: Watu wote tusimame ili tuanze ibada ya kutoa leseni kwa wainjilisti.

55

Kiongozi: Kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu. Kiongozi: Tuombe sala ya Kimya. Kiongozi: Basi nawasihi watu wote tusimame na tuweze kukiri Imani ya Mitume inayotuunganisha na Wakristo wengine ulimwengu. Kiongozi: Nawasihi tukae sote na tuimbe wimbo wa namba……… Kiongozi: Nimkaribishe …………. aongoze maombi. Kiongozi: Ningependa kukaribisha kwaya zifuatazo. Kiongozi: Sasa tutasikiliza neno la Mungu kutoka kwa………. Kiongozi: Wainjilisti wote wanaopokea leseni wasimame. Kiongozi: Sasa nitamkaribisha …………. kwa ajili ya kuwauliza maswali wainjilisti au kama kuna mchungaji anayepokea leseni. Mchungaji: Nitawauliza maswali yafuatayo na ninaomba mujibu kama inavyotakiwa 56

1) Je unamwamini Mungu baba, Mwana na Roho Mtakatifu, nawe unakubali kumkiri upya Bwana Yesu Kristo kuwa Bwana na Mwokozi wa Maisha yako? 2) Je unakubali neno la Mungu lililo katika maandiko ya Agano la Kale na Agano Jipya kwamba ndiyo msingi mkuu wa mafundisho ya kanisa hili? 3) Je unakubali kutii katiba na kanuni za kanisa hili zilizopitishwa na Mkutano Mkuu na kwamba utashirikiana na uongozi katika utekelezaji wake?

Mchungaji: Kwa kuwa mmekubali, basi pigeni magoti mbele za Mungu, na tutaomba pamoja kwa ajili ya kuwakabidhi katika mikono salama ya Mungu wetu. Maelekezo: wachungaji na watu wote wainue mikono yao kuelekea kwa waleseni bila kuweka juu ya vichwa vyao.

Mchungaji: Kulingana na mwito wenu wa kuhubiri Injili, na kwa kutimiza vigezo vya Kibiblia na vile vilivyowekwa na Mkutano Mkuu, ninawatunuku ninyi “cheti cha leseni ya kuhubiri injili kinachotolewa na kanisa letu.” Kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu. Amina. 57

Kiongozi: Sasa nitamkaribisha Katibu wa kamati ya Usimikaji ili awakabidhi vyeti usimikwa. Kiongozi: Wakati huu tutatoa Sadaka na kwaya ya……… wataimba. Kiongozi: Sasa nitakakaribisha watu wafuatao kwa ajili ya kutoa pongezi zao Kiongozi: Nitamkaribisha mchungaji…………. kwa ajili ya kusoma Matangazo Kiongozi: Nawaomba tusimame na tuimbe wimbo wa tenzi namba… Kiongozi: Sasa nitamkaribisha Mch …………kwa ajili ya kutoa baraka. Kiongozi: Tutoke nje kwa utaratibu maalum.

7. Ibada ya Kuweka Wakfu Jengo Maelekezo: ibada hii inaweza kufanyika siku yoyote ile kwa kutegemeana na ratiba ya kanisa husika. Ibada hii itakuwa na sehemu mbili muhimu; nje ya jengo na ndani ya jengo. Ufuatao ni utaratibu wa ibada nje na ndani ya jengo. Vitu vya kuandaa katika kuweka wakfu jengo la kanisa ni; 1) hakikisha kuna maandalizi ya kukata utepe kama ishara ya 58

kuzindua 2) hakikisha kuna Biblia na Vifaa vya meza ya Bwana kama alama za kanisa wakati wa ibada ya ndani)

Nje ya Jengo la Kanisa Maelekezo: watu wakusanyike mbele ya jengo husika na kwa utulivu tayari kwa ajili ya kuanza ibada

Kiongozi:

Karibuni wapendwa katika Bwana mbele ya jengo hili la kuabudia kwa ajili ya kuanza ibada maalum ya kuweka wakfu jengo hili.

Kiongozi: Kwa nyakati zote, Mungu Mwenyezi amewatia moyo watu wake kwa kujenga nyumba za sala na sifa, na kutenga maeneo ya huduma ya Neno lake takatifu na Sakramenti. Kwa heshima kubwa Mbele za Mungu jengo la kanisa hili limekamilika, na sasa tumekusanyika kwa ajili ya kumtolea Mungu sifa na utukufu. Kiongozi: Tuombe: “Mungu Mwenyezi, tunakushukuru kwa kutufanya kwa mfano wako, na kwa kutushirikisha katika kuboresha uumbaji wako. Sasa, Pokea kazi ya mikono yetu mahali hapa, leo ukaitenge 59

nyumba hii kwa ajili ya ibada ninaomba katika jina la Yesu”

yako,

Wote: Amina Kiongozi: Nitamkaribisha………kwa ajili ya kuongoza maombi ya kufungua ibada hii Kiongozi: Nitamkaribisha…… atoe neno kwa ufupi Kiongozi: Sasa ni muda mzuri wa kukata utepe ulioko mbele yetu, na kisha kufungua rasmi jengo hili kwa ishara ya jiwe la msingi Maelekezo: watu watakaokata utepe wanapaswa kuandaliwa mapema ili kusiwepo na mkanganyiko wa kila mtu kutaka kukata utepe.

Kiongozi: Sasa nitamkabidhi funguo ndugu……. kwa ajili ya kufungua rasmi jengo hili. Maelekezo: kiongozi anapaswa apewe funguo mapema na atamkabidhi mtu ambaye amepewa jukumu la kuzindua jengo hilo.

Kiongozi: Basi ninawakaribisha nyote tuingie ndani ya jengo hili kwa ajili ya kuendelea na ibada (wataingia kwa utaratibu maalum wakiongozwa na wachungaji wote). 60

Ndani ya Jengo: Kiongozi: Tukiwa katika hali ya kusimama tuimbe wimbo namba……… Kiongozi: Kwa pamoja tukiri imani ya Mitume. Kiongozi: Tafadhali sote tukae kwenye viti vyetu. Kiongozi: Nitamkaribisha ……kwa ajili ya kusoma Neno la Mungu litakalotuongoza katika mahubiri ya leo. Kiongozi: Nitamkaribisha…………kwa ajili ya kuongoza maombi. Kiongozi: Nitakaribisha kwaya zifuatazo kwa ajili ya kumsifu Mungu (kwaya zote ziandaliwe mapema). Kiongozi: Nitamkaribisha…………. kwa ajili ya kusoma historia fupi ya ujenzi wa kanisa hili. Maelekezo: historia iandaliwe kwa ufupi; gharama za ujenzi ikiwezekana ziwekwe wazi, kuwashukuru wote waliochangia ujenzi nk Kiongozi: Sasa nitamkaribisha……………. kwa ajili ya mahubiri (mahubiri yasizidi dakika 40). Mhubiri: (baada ya kuhubiri) nipende kuwakaribisha wachungaji wote kusogea mbele kwa ajili ya kuweka wakfu jengo hili kwa maombi. (wachungaji watakaofika mbele ni wale tu waliosimikwa na wenye mavazi maalum). 61

Mhubiri: Naomba wachungaji wote tuinue mikono yetu juu kwa ajili ya kuomba na kuweka wakfu jengo hili kwa ajili ya kazi ya Mungu. Mhubiri: (baada ya maombi ya pamoja, Mhubiri ataomba maombi yafuatayo) Maombi. Ee Mwenyezi Mungu tunakushukuru kwa ajili ya ukamilishaji wa ujenzi wa jengo hili. Na sasa Bwana tunakusihi kwamba jengo hili liwe sehemu maalum kwetu kwa kuja kusikiliza neno lako, na kushiriki sakramenti takatifu. Baba pokea kazi ya mikono yetu kama wanadamu, na ipate kibali mbele za Macho yako; Bwana Yesu Kristo, fanya hekalu hili kuwa uwepo wako na nyumba ya sala. Kuwa karibu nasi kila wakati tunapokutafuta katika mahali hapa. Sasa Jengo hili ninaliweka Wakfu kwa jina la Baba, na la Mwana na la Roho Mtakatifu. Washirika: Amina Mhubiri: Ningependa kumtambulisha mchungaji wa kanisa la mahali hapa. Naomba apite mbele yeye na familia yake (kama kanisa ni jipya, basi atakaribisha na washirika wapya wa kanisa hilo kwa ajili ya kuwaombea) 62

Mhubiri: Ninaomba watumishi wote tuinue mikono yetu juu ya mtumishi wa kanisa hili pamoja na familia yake ili tuwakabidhi mbele za Mungu kwa ajili ya huduma ya mahali hapa. Mhubiri: Sasa tutakabidhi alama za kanisa kwa mchungaji, tayari kwa ajili ya kuendelea na huduma rasmi katika kanisa hili. Maelekezo: Alama za wazi za kanisa ni neno (Biblia) na Sakramenti (vyombo vya Meza ya Bwana) kama ishara ya kanisa letu. (vifaa hivi viandaliwe mapema, na atakabidhiwa mchungaji husika

Kiongozi: Ninapenda kukaribisha Shukrani kutoka kwa……

Neno

la

Kiongozi: Tusikilize matangazo kutoka kwa……… Kiongozi: Tusimame sote na tuimbe wimbo wa …… Kiongozi: Nimkaribishe mchungaji……… kwa ajili ya kutoa baraka Kiongozi: Sote tutoke kwa utaratibu maalum tukiongozwa na wachungaji wote.

63

8. Kuweka Wakfu Vifaa vya Kanisa Maelekezo: Kanisa au muumini anaponunua kitu chochote kwa ajili ya kazi ya Mungu, ni vizuri kukiweka wakfu. Kuweka wakfu maana yake ni kukitenga kutokana na matumizi ya kawaida. Ibada hii kwa kawaida hufanyika ndani ya ibada ya Jumapili.

Kiongozi: Kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu Washirika: Amina Kiongozi:

Tunamshukuru Mungu kwa ajili ya upatikanaji wa……..na muda huu tutakiweka Wakfu kwa ajili ya matumizi maalum ndani ya kanisa hili.

Kiongozi: Tuimbe wimbo wa………… Mchungaji: Tungependa kusikiliza historia ya upatikanaji wa vifaa hivi. Mchungaji: Tusikilize neno (mahubiri mafupi. Kuhusu vifungu vya dharura vya kuhubiri rejea uk. 88)

64

Mchungaji:

Watu wote tusimame kwa ajili ya maombi maalum ya kuviweka wakfu kifaa/vifaa hivi.

Mchungaji: Ee Mwenyezi Mungu uliye mpaji wa vitu vyote, Asante kwa ajili ya vifaa hivi ambavyo vimewekwa mbele zako kwa ajili ya matumizi maalum ya kazi yako. Na sasa ninaviweka Wakfu rasmi kwako, kwa ajili ya matumizi kanisa hili. Kuanzia sasa vifaa hivi vitakuwa vimetengwa kwa ajili ya kazi yako tu. Vilevile ninakushukuru kwa ajili ya watumishi wako ambao wamejitolea mali zao kwa ajili ya kufanikisha ununuzi wa vifaa hivi, Ee Mwenyezi Mungu ukawabariki na kuzidi. Waongezee zaidi mahali walipotoa. Na sasa naviweka wakfu vifaa hivi, kwa jina la Baba, na Mwana na Roho Mtakatifu. Mchungaji: wakati huu tutaomba kwa ajili ya watu walijitolea kutoa vifaa hivi kwa ajili ya kazi ya Mungu. (kanisa zima wanaweza kuomba pamoja, halafu mchungaji unamalizia)

Washiriki: Amina 65

Mchungaji: Neema ya Bwana Wetu Yesu Kristo na Upendo wa Mungu Baba na Ushirika wa Roho Mtakatifu ukae nanyi nyote sasa na hata milele Washirika: Amina Mchungaji:

Huu ndio mwisho wa ibada hii. Nakaribisha ratiba zingine ziendelee.

9. Ibada ya Mahafali ya Chuo cha Biblia Maelekezo: Wanafunzi wapangwe kwa kuzingatia alfabeti za kwanza za majina yao ya mwisho ili kuleta mpangilio mzuri wa ukaaji. Wanafunzi watatangulia mbele wakifuatiwa na wachungaji.

Kiongozi: Naomba wahitimu na wachungaji uingie sasa ili tuanze ibada yetu. Wakati huo tutakuwa tunaimba wimbo………… Kiongozi: Kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu Wote: Amina Kiongozi: Tuombe sala ya Kimya (kama dakika moja hivi, baada ya sala ya kimya kiongozi ataomba kwa sauti kubwa)

66

Kiongozi: Basi nawasihi tuweze kukiri Imani ya Mitume inayotuunganisha na Wakristo wengine ulimwengu. Kiongozi: Nawasihi tukae sote na tuimbe wimbo wa namba……………… Kiongozi: Nimkaribishe Mchungaji ……aongoze maombi. Kiongozi: Ningependa kukaribisha kwaya zifuatazo: Kiongozi: Sasa tutasikiliza neno la Mungu kutoka kwa………… Kiongozi: Sasa ni wakati wa kutambulisha wageni Maelekezo: Ni lazima uwe na majina ya wageni mezani kwako na kuwataja kwa majina yao, nao watasimama na kupunga mikono. Epuka kueleza sana juu ya wageni hao kwani unaweza kukosea taarifa zao.

Kiongozi: Sasa nimkaribishe Mkuu wa chuo kwa ajili ya kutaja majina ya wahitimu wa leo. (kila atakayetajwa atasimama) Kiongozi: Sasa nimkaribishe……..…kwa ajili ya kusoma historia fupi ya chuo chetu.

67

Kiongozi: Sasa tutasikiliza risala kutoka kwa wanafunzi. Kiongozi: Sasa nimkaribishe Mkuu wa Chuo kwa ajili ya kutoa hotuba yake. Kiongozi: Sasa nimkaribishe tena Mkuu wa Chuo kwa ajili ya kumkaribisha mgeni rasmi atoe hotuba yake. Maelekezo:

Mkuu wa chou aeleze kwa ufupi kuhusu mgeni huyo rasmi; kwa mfano kazi yake, elimu yake, ushawishi wake, mafanikio yake, nk. Lengo la mgeni rasmi ni kuwatia moyo wanafunzi kupitia pia uzoefu wake.

Kiongozi: Nimkaribishe mgeni rasmi/mkuu wa chuo kwa ajili ya kutoa vyeti kwa wahitimu. Maelekezo: Upigaji wa picha utazingatia mazingira ya tukio. Kiongozi anapaswa atoe maelekezo namna ya upigaji wa picha.

Kiongozi: Kipindi hiki ni kwa ajili ya Wahitimu kutoa zawadi kwa Chuo Maelekezo:

ikiwezekana uongozi wa chuo uione zawadi mapema kabla ya tukio ili kuepusha mikanganyiko inayoweza kujitokeza. 68

Kiongozi:

Kipindi watatoa

hiki wanafunzi zawadi kwa

(mwanafunzi mmoja wawakilishe wenzao)

au

wanaobaki wahitimu

wachache

tu

Kiongozi: Kipindi hiki uongozi wa chuo watatoa zawadi kwa wahitimu Maelekezo: chuo kinaweza kuchagua wanafunzi wachache waliofanya vizuri katika masomo yao katika nyanja mbalimbali, mfano; nidhamu, masomo nk.

Kiongozi: Sasa tusikilize maneno ya pongezi kutoka kwa watu wafuatao: Maelekezo: watakaotoa pongezi wanapaswa kuandaliwa mapema, na wanapaswa wasianze kuhubiri tena katika pongezi zao; dakika 1-2 zinatosha kwa kila mmoja.

Kiongozi: Nitamkaribisha mchungaji……kwa ajili ya kusoma Matangazo. Kiongozi: Nawaomba tusimame tuimbe wimbo namba……. ubeti moja na korasi yake. Kiongozi: Sasa nitamkaribisha Mchungaji…….kwa ajili ya kutoa Baraka. Kiongozi: Tutoke nje kwa utaratibu maalum.

69

10.

Ibada ya Mahafali ya Shule ya Awali, Msingi na Sekondari

Maelekezo:

shule za Kikristo zina lengo la kuwanufaisha wanafunzi kwa kuwapa ufahamu wa elimu dunia na elimu ya neno la Mungu. Wanapofikia hatua ya kuhitimu, basi linakuwa ni jambo la kumshukuru Mungu, na kwamba siku ya mahafali yao ni sehemu ya ibada kwa kumtukuza Mungu.

Kiongozi: Naomba wahitimu na waalimu uingie sasa ili tuanze ibada yetu ya mahafali. Maelekezo: wanaweza kuingia kwa wimbo wa kitabuni au ala ya mziki. Kamwe hairuhusiwi kuingia kwa kutumia mziki wa kidunia. Wanafunzi wapangwe kwa kuzingatia alfabeti za kwanza za majina yao ya mwisho ili kuleta mpangilio mzuri wa ukaaji. Wanafunzi watatangulia mbele wakifuatiwa na wachungaji.

Kiongozi: karibuni ndugu zangu wapendwa katika Mahafali ya…………. ya Shule yetu. Kwa kuwa tulianza na Mungu, basi tunaenda kumaliza na Mungu tena siku ya leo. Kiongozi: kwa jina la Baba, na la Mwana na la Roho Mtakatifu 70

Watu wote: Amina Kiongozi: Tuombe (kiongozi aombe) Kiongozi: Nakaribisha vikundi cha kwaya kilichoandaliwa kwa ajili ya kufungua mahafali haya. Kiongozi: Sasa tutasikiliza neno la Mungu kutoka kwa……………… Kiongozi: Baada ya mahubiri haya, sasa shughuli ya mahafali inaendelea Kiongozi: Nitakaribisha vikundi vifuatavyo kwa ajili ya nyimbo (wimbo kutoka kwa wale wanaobaki, wahitimu, na waimbaji wengineo)

Kiongozi: Huu ni wakati wa utambulisho Maelekezo: Mwalimu mkuu/kiongozi wa shule/ au mtu mwingine yeyote yule anaweza kutambulisha wageni. Ni lazima uwe na majina ya wageni mezani kwako na kuwataja kwa majina yao, nao watasimama na kupunga mikono. Epuka kueleza sana juu ya wageni hao kwani unaweza kukosea taarifa zao.

Kiongozi: Sasa nimkaribishe….………kwa ajili ya kusoma historia ya shule (mwanafunzi au mwalimu atasoma historia hiyo) 71

Kiongozi: Sasa tutasikiliza risala kutoka kwa wanafunzi Maelekezo:

Mwanafunzi mmoja au wawili wawakilishe wengine katika kusoma. Inapendekezwa kwamba mwalimu apate nakala ya risala mapema.

Kiongozi: Sasa nimkaribishe………kwa ajili ya hotuba Kiongozi: Sasa nimkaribishe tena……kwa ajili ya kumkaribisha mgeni rasmi kutoa hotuba yake. Maelekezo: Mwl Mkuu au mkurugenzi au meneja au kiongozi yeyote yule anayehusika atapaswa kuelezea kidogo kuhusu mgeni huyo rasmi; kwa mfano kazi yake, elimu yake, ushawishi wake, mafanikio yake, nk. Lengo la mgeni rasmi ni kuwatia moyo wanafunzi kupitia pia uzoefu wake.

Kiongozi: Nimkaribishe…………kwa ajili ya kumkaribisha tena mgeni rasmi kwa ajili ya kutoa vyeti kwa wanafunzi. Maelekezo: Utoaji wa vyeti ni kwa watoto wa shule ya awali. Kwa wanafunzi wa shule ya msingi ni wale tu waliofanya vizuri. Hata hivyo shule inaweza kuamua kuwapa wanafunzi vya kumaliza katika shule hiyo kwa kuzingatia.

72

Kiongozi: Kipindi hiki ni kwa ajili ya Wahitimu kutoa zawadi kwa waalimu (ikiwezekana uongozi wa shule uione zawadi mapema kabla ya tukio)

Kiongozi: Kipindi hiki wanafunzi wanaobaki watatoa zawadi kwa wahitimu (mwanafunzi mmoja au wachache tu wawakilishe wenzao)

Kiongozi: Kipindi hiki uongozi wa shule utatoa zawadi kwa wahitimu Maelekezo: Shule kinaweza kuchagua wanafunzi wachache waliofanya vizuri katika masomo yao katika nyanja mbalimbali, mfano; nidhamu, masomo nk.

Kiongozi: Sasa tusikilize maneno ya pongezi kutoka kwa watu wafuatao: (kwa mfano mwenyekiti wa bodi ya shule, mzazi mwakilishi, na wengineo ambao watakuwa wameandaliwa mapema)

Kiongozi: Nitamkaribisha……kwa ajili ya kusoma Matangazo Kiongozi: Sasa nitamkaribisha Mchungaji……...kwa ajili ya kutoa baraka. (mwisho wa ibada)

73

V. IBADA ZA SIKUKUU ZA KANISA Ibada maalum ni zile ibada ambazo zinafanyika mara chache, kwa kuzingatia ratiba zilizowekwa. Zifuatazo ni ibada ambazo zitakuwa maalum kwa kanisa letu: -

1. Ibada ya Siku ya Kwanza ya Mwezi Kila siku ya kwanza ya mwezi kutakuwepo na ibada ya maombi kwa Wakristo wote. Kila kanisa la mahali litapaswa kupanga namna maombi hayo yatakavyofanyika. i. ii. iii.

iv.

v.

Ibada hii itaendeshwa kama ibada ya Jumapili Ibada hii itafanyika asubuhi au jioni kwa kutegemea na makubaliano ya kanisa husika; Wakristo wote wanakumbushwa kujiandaa kikamilifu kwa ajili ya kumshukuru Mungu kwa mwezi uliopita na kuanza mwezi mwingine na Bwana. Kama mchungaji yupo, basi ni vizuri kushirikisha Meza ya Bwana hata kama ni asubuhi ili kujenga umoja wa kanisa. Kiongozi ahakikishe kwamba watu wanapata muda wa kutosha kumwomba Mungu. 74

2. Ibada ya Krismasi i. Kutakuwepo na ibada ya Krismasi ambayo ni kukumbuka kuzaliwa kwa Bwana wetu Yesu Kristo hapa duniani. ii. Hii itakuwa ni ibada pekee ambayo itaambatana na kumshukuru Mungu kwa zawadi ya Bwana wetu Yesu Kristo. iii. Kama ilivyo desturi, ibada hii hufanyika tarehe 25 Desemba kwa kila mwaka. Kuhusu muda itategemea kanisa la mahali litakavyoamua. iv. Kanisa linaweza kutumia kipindi hiki kwa ajili ya uinjilisti, yaani kwa kuwaleta watu wengine kwa Yesu. Inawezekana kufanya mikutano ya Injili, pamoja na shughuli zingine za kikanisa zenye mlengo wa kuinjilisha.

3. Ibada ya Mwaka Mpya i. Kutakuwepo na ibada maalum kila Januari 1. Ibada hii itahusika na shukrani kwa ujumla. ii. Waumini wote watapata nafasi ya kumshukuru Mungu kwa maombi na sadaka. iii. Watu watakaopenda kushuhudia matendo makuu ya Mungu kwa mwaka uliopita 75

watapata nafasi ya kufanya hivyo ikiwa watatoa taarifa mapema. iv. Kwa kuzingatia kanisa la mahali husika, inawezekana kuwepo kwa mkesha wa mwaka mpya, lakini si lazima. v. Kwa makanisa yatakayokuwa na mkesha, basi wanapaswa kuzingatia muda wa kumaliza mkesha ili watu wapate nafasi asubuhi kuja kumwabudu Mungu kwa pamoja.

4. Ibada ya Pasaka i. ii.

iii.

Kutakuwepo na ibada maalum Jumapili ya pasaka kwa kila mwaka. Ibada ya pasaka inaweza kufanyika kuanzia siku ya Ijumaa kwa ajili ya kukumbuka mateso ya Bwana Wetu Yesu Kristo (yaani siku ya Ijumaa Kuu) Kutakuwepo na Meza ya Bwana katika ibada hii, hivyo washirika wote wanapaswa kuandaliwa vizuri.

5. Ibada ya Jumapili ya Siku ya Matengenezo i. Matengenzo ya kanisa yalianza mwanzoni mwa karne ya 16, kwa kupinga mafundisho ya uongo yaliyofundisha na 76

Kanisa Katoliki; mwaka unaotambulika rasmi ni 1517. ii. Tukio hili linakumbukwa kwa sababu lililitoa kanisa kutoka kwenye uhamishoni Babeli (Calvin 1509 –1564) iii. Kwa kawaida inakuwa ni Jumapili ya mwisho ya mwezi wa Oktoba iv. Matukio mbalimbali yanayohusu matengenezo ya kanisa yatakuwepo (kwa mfano maigizo, ngojera, na mengineyo v. Kuanzia Jumatatu kuelekea Jumapili ya Matengenezo kutakuwepo na warsha mbalimbali kuzungumzia historia ya matengenezo; kanisa litachagua mada ya matengenezo siku hiyo.

Utaratibu wa ibada Jumapili ya Siku ya Matengenezo Maelekezo: Utaratibu huu ni mwongozo tu; hata hivyo kuna mambo mengi yanaweza kufanywa katika Jumapili hii. Hata hivyo mambo yaliyopo kwenye utaratibu ndiyo mambo ya msingi.

Kiongozi: Leo ni Jumapili ya kukumbuka Matengenezo ya Kanisa. Kiongozi: “Wewe, BWANA, nguvu zangu, nakupenda sana; BWANA ni jabali langu, na boma langu, na mwokozi wangu.” (Zab. 18:1-2) 77

“Lakini

yeye alisema, Afadhali, heri walisikiao neno la Mungu na kulishika.” (Lk. 11:28) “Kwa maana siionei haya Injili; kwa sababu ni uweza wa Mungu uuletao wokovu, kwa kila aaminiye, kwa Myahudi kwanza, na kwa Myunani pia. Kwa maana haki ya Mungu inadhihirishwa ndani yake, toka imani hata imani; kama ilivyoandikwa, Mwenye haki ataishi kwa imani.” (Rumi 1:16-17) “Ninyi

mkikaa katika neno langu, mmekuwa wanafunzi wangu kweli kweli; 32tena mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru.” (Yn. 8:31b-32) “Lakini

Mungu na ashukuriwe atupaye kushinda kwa Bwana wetu Yesu Kristo. Basi, ndugu zangu wapendwa, mwimarike, msitikisike, mkazidi sana kutenda kazi ya Bwana sikuzote.” (1Kor. 15:57-58b) Ee Mwenyezi Mungu, Muumba Mbingu na Nchi, tunakushukuru kwa kuwa wewe ni Mungu wa historia. Katika Historia tumeona namna watumishi wako walivyosimama kutetea Imani ya Kikristo. Pale wazushi walipohatarisha usalama wa kanisa, watumishi wako walisimama imara. Jumapili ya leo tunakumbuka tukio muhimu katika historia ya kanisa. Tunakuomba uwe pamoja nasi, tunaomba katika Jina la Yesu Kristo. 78

Washirika: Amina Kiongozi: Tukiwa hali ya kusimama nitasoma imani ya mitume ya Nikea (kiongozi usome na mwisho watu kusema)

wote

watakubaliana

kwa

Kiongozi: Nawasihi tukae na tuimbe wimbo namba 71 “Mteteeni Yesu” Kiongozi: Naomba mtu aliyeandaliwa kwa ajili ya maombi aombe. Kiongozi: Huu ni wakati wa kusoma neno la Mungu ambalo litatuongoza katika mahubiri ya leo. Kiongozi: Sasa tutasikiliza na kuona matukio mbalimbali kuhusu Matengenezo ya Kanisa. Maelekezo: matukio haya yanaweza kuwa maigizo, ngojera, mashairi, nk Kiongozi: Huu ni wakati wa kusikiliza neno la Mungu kutoka kwa…………. Kiongozi: Ni wakati wa kutoa sadaka. Wakati huu kwaya itaimba wimbo/nyimbo………

79

Kiongozi: Ni wakati wa kusikiliza matangazo ya leo. Namkaribisha asome Matangazo. Kiongozi:

Tusimame namba…

sote

na

tuimbe

wimbo

Kiongozi: Ni wakati wa kupokea baraka za Mungu.

80

VI. IBADA ZA IDARA ZA KANISA Idara mbalimbali za kanisa zimepewa vipaumbele kuwepo na ibada maalum katika Jumapili moja kwa mwaka.

1. Juma la Wanawake a) Itafanyika mara moja kwa mwaka b) Itakuwa katika Juma la kwanza kwa mwezi wa tatu (3) c) Viongozi wa ibada watakuwa wanawake na wataongoza matukio yote ndani ya kanisa d) Shughuli zote zitakazoendeshwa ndani ya kanisa kwa mujibu wa utaratibu wa ibada hii ziandaliwe mapema. e) Kuhusu utaratibu wake wa ibada Rejea “utaratibu wa ibada za idara” uk. 82

2. Juma la Wanaume a) Ingawa wanaume mara nyingi ndio huongoza matukio katika ibada mbalimbali makanisani, lakini kutakuwepo na Juma la wanaume b) Litakuwa Juma la pili kwa mwezi wa kumi (10)

81

c) Matukio yote yatakayofanyika katika ibada yaandaliwe mapema na kwa utaratibu mzuri; d) Kuhusu utaratibu wa ibada, rejea “utaratibu wa ibada za idara.” Uk. 82

3. Juma la Vijana a) Viongozi wa idara ya vijana watawajibika kuandaa na kuongoza ibada hii; b) Itakuwa katika Juma la pili kwa mwezi wa pili (2) c) Kuhusu utaratibu, rejea “utaratibu wa ibada za idara.”uk. 82

4. Juma la Watoto a) Mwinjilisti wa watoto atawajibika kuandaa matukio yote yanayopaswa kufanyika katika ibada hii b) Itakuwa katika Juma la pili kwa mwezi wa sita (6) c) viongozi wa idara wataongoza ibada hii (kwa mfano Mwinjilisti wa watoto, waalimu wa watoto nk) d) ibada hii inaweza kuambatana na kongamano ambalo litamalizika katika Jumapili hii. 82

e) Matoleo katika ibada hii yatatumika kwa ajili ya idara ya watoto. f) Kuhusu utaratibu wa ibada hii rejea “utaratibu wa ibada za idara.”uk. 82

Utaratibu wa Ibada za Idara Maelekezo: Ibada za makundi maalum zitaongozwa na makundi hayo kwa kuzingatia matakwa ya viongozi wa ibada kwa ujumla. Ibada hizi zitakuwa na maandamano mafupi yanayoanzia nje ya kanisa na kuelekea ndani ya kanisa. Matukio yote yataongozwa na makundi hayo isipokuwa Ibada katika Juma la Watoto.

Kiongozi: Ninaomba sasa msafara wa maandamano uingie ndani ya kanisa Kiongozi: Tukiwa katika hali ya kusimama, tutulie mbele za Bwana kwa ajili ya kuanza ibada yetu Kiongozi: Kwa jina la Baba, na la Mwana, na la Roho Mtakatifu Washiriki: Amina Kiongozi: Siku ya leo ni Jumapili ya………ambapo tumekutana kumshukuru Mungu na kumtukuza yeye; kwa hiyo ibada ya leo 83

itaongozwa na viongozi ya……… Karibuni nyote.

wa

idara

Kiongozi: Tuombe kwa ajili ya kuanza ibada Maelekezo: Soma zaburi inayoendana na tukio la siku hiyo bila kutaja kwamba ni Zaburi ipi, halafu ukimaliza kusoma omba moja kwa moja bila kupumzika.

Kiongozi: Nawasihi tukiri Imani ya Mitume inayotuunganisha na Wakristo wengine wote ulimwenguni Kiongozi: Tukiwa katika hali ya kukaa, tuimbe wimbo namba……….. Kiongozi: Sasa nitamkaribisha…………..kwa ajili ya kuongoza maombi Kiongozi: Sasa tutasikiliza nyimbo kutoka idara… Kiongozi: Sasa tutasikiliza neno la Mungu kutoka kwa…………… Kiongozi: sasa ni wakati wa kutoa Matoleo; kwaya ya idara itaimba nyimbo wakati wa kutoa. Maelekezo: Inapendekezwa nusu ya matoleo haya yaelekezwe kwenye idara husika, hata 84

hivyo kila vinginevyo.

kanisa

linaweza

kuamua

Kiongozi: sasa tutasikiliza na kuona matukio mbalimbali yaliyoandaliwa na idara……. katika ibada hii Maelekezo: Yanaweza kuwa ngonjera, mashindano ya kukariri, kuonyesha vipaji, kubariki watumishi kwa zawadi, kutoa chochote kwa kanisa, nk.

Kiongozi: sasa nitamkaribisha…………kwa ajili ya pongezi kwa idara; Kiongozi: Ni wakati wa kusikiliza matangazo ya leo (haya ni matangazo ya jumla, hivyo viongozi wa kanisa watatangaza) Kiongozi: Tusimame sote; tuimbe wimbo namba… Kiongozi: Nitamkaribisha mchungaji kwa ajili ya baraka.

85

VIFUNGU VYA MSAADA Vifungu vifuatavyo vinaweza kutumika katika mahubiri au marejeleo katika ibada husika. Si vifungu vyote vimeorodheshwa, hivyo hivi vilivyoorodheshwa kama dharura kwa mtumiaji. Kuhusu Ibada ya Jumapili; Zaburi. Zab. 7:17; Zab. 8:1-9; Zab. 9:1-2; Zab. 9:9-11; Zab. 18:1-3; Zab. 19:1-6; Zab. 24:1-5; Zab. 28:6-7; Zab. 29:1-2; Zab. 33:1-3; Zab. 33:11-12; Zab. 34:1-3; Zab. 36:5-7; Zab. 40:4-5; Zab. 42:1-2; Zab. 46:1-3; Zab. 47:1-2; Zab. 57:9-11; Zab. 61:1-2; Zab. 63:1-3; Zab. 66:1-4; Zab. 67:1-5; Zab. 68:34-35; Zab. 69:3034; Zab. 72:18-19; Zab. 84:1-4; Zab. 84:8-12; Zab. 86:8-10; Zab. 89:5-8; Zab. 91:1-2; Zab. 92:1-4; Zab. 93:1-4; Zab. 95:1-3; Zab. 95:6-7; Zab. 96:1-3; Zab. 96:7-9; Zab. 96:11-13; Zab. 98:1-3; Zab. 98:4-6; Zab. 99:1-3; Zab. 100:1-5; Zab. 103:1-5; Zab. 103:19-22; Zab. 104:1-2; Zab. 104:31-34; Zab. 105:1-3; Zab. 106:1; Zab. 107:1-3; Zab. 108:1-4; Zab. 111:1-3; Zab. 113:1-3; Zab. 117:1-2; Zab. 118:1-4; Zab. 118:24-26; Zab. 130:5-8; Zab. 134:13; Zab. 135:1-3; Zab. 136:1-3; Zab. 138:1-2; Zab. 145:1-3; Zab. 146:1-2; Zab. 147:1-5; Zab. 147:7-11; Zab. 148:1-6; Zab. 148:7-13; Zab. 149:1-5; Zab. 150:1-6 Kuhusu Ibada ya Ubatizo Mt. 28:19, Gal. 3:27, Mk 1:4; Ufu. 1:5, Tit. 3:5; Efe. 5:26, Gal. 3:26-27, I Kor. 15:29; Rum 6:5, I Kor. 12:13, 86

Rum. 6:4. Kuhusu wanaostahili kubatizwa Mdo 2:38; 8:36-37, Mwa. 17: 7, 9; Gal. 3:9, 14; Kol. 2:11-12; Mdo 2:38-39; Rum. 4: 11-12; 11:16;1 Kor. 7:14; Math. 28:19; Lk 18:15-16 Kuhusu Ibada Meza ya Bwana Lk 22:20, Mt. 26: 26-28; 1 Kor. 11: 13-26, 1 Kor. 10:16, 1 Kor. 11:24, 1 Kor. 10: 14-16, 21, 1 Kor. 10:17, Mdo 3:21, 1 Kor. 11: 24-29 (kuhusu watu wenye kashfa 1 Kor. Sura. 5; 11: 27-31; Mt. 7:6; Yud. 1: 23; I Tim. 5:22 II Kor. 2:7 Kuhusu Ibada ya Maombi Zab. 62: 8, Yn. 16:23, Rum. 8:26, Zab. 32: 5-6; Dan. 9: 4, Fil. 4: 6, Dan. 10:2, 1) I Fal. 8:39; Mdo 1:24; Rumi 8:27, Zab. 65: 2, Mika 7:18, Zab. 145: 18-19, Rum. 10:14, Mt. 4:10, Zab. 50:15, Rum. 8: 26-27; Zab. 10:17; Zek. 12:10, 1) Efe. 6:18; Zab. 28: 9 I Tim. 2: 1-2, Kol. 4: 3, Mwa. 32:11, Yak. 5:16, Mt. 5:44, I Tim. 2: 1-2, Yn. 17:20; II Sam. 7:29, II Sam. 12: 21-23, I Yn. 5:16. Vitu tunavyopaswa kuviomba Mt. 6: 9, Zab. 51:18, 122: 6, Mt. 7:11, Zab. 125: 4, I Yoh. 5:14. Tupasavyo kuomba Lk 15: 17-19 Lk 18: 13-14, Zab. 51:17, Fil. 4: 6, II Sam. 1:15, 2: 1, I Kor. 14:15, Mk. 11:24; Yak. 1: 6, Zab. 17: 1; 145: 18, Yak. 5:16, I Tim. 2: 8, Efe. 6:18, Mik, 7: 7, Mt. 26:39, Mt. 6: 2-13; Lk. 11: 2-4. Kuhusu Ibada ya Ndoa Mwa 2:23-24, 1 Kor 7:2,39, Mt 19:4-6, Efe 5:28,31,33, 1 Kor 13:8,13, Mt 5:31-32, Mk 10:5-9, Rum 7:2-3. Ndoa ilivyoanzishwa na makusudi yake Mwa 2:18,24, 87

Mwa 1:27-28, Efe 5:22-23, Kol 3:18-19, Mwa 2:18-25, 1 Kor 7:3-5, 9,36, Mwa 1:27-28, 9:1, Mal 2:15, Mt 18:5-6,10,14, 19:14, Efe 6:1-4, Kol 3:20-21, Mk 10:1316, Lk 18:15-17. Mipaka katika ndoa na mengineyo Mwa 1:27-28, Mk 6:18, 1 Kor 5:1, Law 18:6-18, Mk 1:30, Yn 2:1-2, 1Tim 5:14, Ebr 13:4, 1 Kor 7:7,36, 9:5, 1 Tim 4:3, 1 Kor 7, hasa mstari wa 39, 2 Kor 6:14-15. Mith 18:22, Mt 19:6, Efe 5:29-30, 32, Mk 10:9, 11-12, Mk 10:9. Kuhusu Ibada ya Mazishi 2 Sam. 12:16-17; Ayu. 14:14; Zab. 23:4; Rum. 8:35, 37-39; Zab. 39:4; 48:14; 116:15; 146:4; Mith. 14:32; Mhu. 3:1-4; Isa. 25:8; 57: 1-2; Yoh. 14: 1-3; Mhu. 3: 14; 1 Thes. 4: 14-17; 2 Kor. 1:3-4; 15:20-23; 15:55-57; Fil. 1: 21-23. Ufu. 1:18; 2:10; 14:13. Kuhusu Ibada ya Kusimika Wachungaji 1 Tim. 4:14, Law. 1: 4; 3: 2-13; 4: 4-33; 8:14, 18, 22; 16:21, (Hes. 27: 18-23; Kum. 34: 9, Mwa. 48: 13-20; 2 Wafalme 13:16; Ayubu 9:33; Zab. 139:5, Mdo 13: 3, Mdo 8:17, Law., Law.1:4, Yn. 17:15. Kuhusu Ibada ya Kutoa Kibali Cha Kuhubiri (Leseni) Efe. 4:11, I Thes. 2:4, I Sam. 2:26, Mith. 8:35, Ezr. 6:14, Isa. 43:9, Neh. 6:7, Math. 4:7, Zab. 64:9, Ezek. 34:2, Mk. 6:12, 16:20, Isa. 60:1-6, Yer. 1:5. Kuhusu Ibada ya Kuweka Wakfu Jengo 2 Sam. 7:5-7, 2 Nyak. 7:16, Zab. 100:4, Mat. 16:18, Isa. 66:1-2, 2 Sam. 7:1-13, Zab. 127:1, 2 Nyak. 7:14, Hag. 2:9, Kumb. 28:8, Zab. 30:1, 2 Nyak. 5:12-14, Ezr. 88

3:10-11, Kumb. 11:18-20, Neh.12:27-47. Ezr. 6:16-17, I Fal. 8:63, Kuhusu Ibada ya Kuwekwa Wakfu Vifaa 1 Nyak. 26:26, 2 Sam. 8:11, Yak. 1:17, Kuhusu Ibada ya mahafali ya shule/vyuo Isa. 58:11, Mith. 4:13, 9:9, 10:4, 2 Tim 6:20, Ayu. 11:12, 1 Tim.4:12, Yos. 1:7-9, Yak. 1:12 Mith 16:3, Fil. 1:6, Mith. 3:5-10, Kol.3:23, Fil. 3:13-14, Fil.1:9-11, Rum. 8:28 Kuhusu Ibada ya Siku ya kwanza ya Mwezi na Mwaka Mpya 1 Kor. 10:22, 31, Zab. 96: 1-3, Isa. 43:18-19. Mal. 4:2, Yer. 29:11, Zab. 121:1–8, Ez. 36:26. Isa. 66:23, Ez. 46:1, Omb. 3:22-24, Mh. 3:11, Efe. 4:22-24, Zab. 35:18, 69:30, 95:1-3, 100:4-5, 106:1. Zab. 90:12 Kuhusu Ibada ya Krismasi Mat. 1:21, 23; Yn, 3:16Gal. 4:4-5, 1 Tim.1:15-17, Isa. 7:14, Isa. 9:6, Tit. 3:3-7, Lk. 2:17-20, Mdo. 5:31, 20:35, Yn. 1:14, 2Kor. 9:15 Lk. 1:37, Rum 15:13, Yn. 1:17, Isa. 11:1, 10, Mwa 3:15; Isa. 42: 6; Yn 6:27, I Yn 5: 11-12, Ebr. 4:15; 7:26, Yn 3:34; Zab. 45: 7, Yn 6:27; Mt. 28: 18-20, Mdo 3: 21-22; Lk 4:18, 21; Ebr. 4: 1415; 5: 5-7; Zab. 2: 6; Mt. 21: 5; Isa. 9: 6-7; Fil. 2: 8-11. Kuhusu Ibada ya Pasaka Kut. 12:11, 43, 44, 45, 48; 1 Kor. 5:7; Ebr. 11:28; Fil. 2: 6-8; Lk 1:31; II Kor. 8:9; Mdo 2:24; Mt. 27: 4; Mt. 26:56; Isa. 53: 2-3; Mt. 27: 26-50; Yn 19:34; Lk 22:44; 89

Mt. 27:46; Isa. 53:10; Fil. 2: 8; Ebr. 12: 2; Gal. 3:13; 1 Kor. 15: 3-4; Zab. 16:10; Mdo 2: 24-27, 31; Rum 6: 9; Mt. 12:40; 1 Kor. 15: 4; Mk 16:19; Efe. 1:20; Mdo 1:11; 17:31 ufufuo Kristo Mdo 2:24, 27 Lk 24:39; Rum. 6: 9; Ufu. 1:18; Yn 10:18; Rum. 1: 4; Rum. 8:34; Ebr. 2:14; Rum. 14: 9; Efe. 1:20, 22-23; Kol 1:18; Rum. 4:25; 1 Kor. 15: 25-27; 1 Kor. 15:20 Kuhusu Ibada ya Jumapili ya Matengenezo Vifungu vinavyohusiana na Siku ya Matengenezo ni vile ambavyo wanamatengenezo walikaza kwa ajili ya kurudisha mafundisho ya kanisa. Rum 1:17; Efe. 2:8;1 Pet. 2:5 2 Tim. 3:16 Mat. 11:29-30, Gal. 2:16, Rum. 3:28, Efe. 2:8-10. Vifungu vingine vinavyohusu zoezi zima la matengenezo: Eze. 22:30, 2 Fal. 22:5, Ezr.9:9 Neh. 4:1nk. Isa. 43. Zak. 10. Neh. 13:14. Kuhusu Juma la Wanawake Mwa. 1:27 Zab. 68:11, Est. 2-8, Isa. 32:11, Yer. 2:33; 9:17, 1 Tim. 2:11-12, 1 Sam. 25:3; Yer. 31:22; Amu. 4:4, 5; Amu. 16:4, 5. 1 Sam.1:1, 2, 4-7; Amu. 4:17-21. 1 Fal. 18:4, 13; 19:1-3; Mwa. 29:20-29. Lk10:38-42; Lk1:26-33; Kut. 15:1, 20, 21; Yosh. 2:1-24; 6:25; Rut. 1:1-6, 15; Mwa.18:20; 19:1, 12, 13; Mdo 17:4; Lk 8:23; I Kor. 11:3; Mith. 31:1-31; Rum. 16:1-27. Kuhusu Juma la Wanaume Mwa. 2:18; 1 Tim. 3:4; 1 Pet. 3:7; Efe. 5:25; 2 Tim. 3:17; 1 Tim. 2:8; 1 Kor. 11:3; Efe. 6:4.

90

Kuhusu Juma la Vijana 1 Tim. 4:12; Mhu. 11:9; Yer. 1:4-8; Mhu. 12:1; Zab. 119:9; 2 Tim. 2:22; Yer. 29:11; Zab. 144:12; Efe. 4:29; 1 Sam.17; Mwa. 37-38; 2 Fal. 5; Mat. 9:20-22; Mdo 20:9; Yosh. 6:23; 1 Yoh. 2:13, 14; 1 Pet.5:5; 1 Tim. 5:11; Mdo. 2:17; Zek.9:17; Yoe. 2:28; Isa. 40:30; Mith. 20:29; Ayu. 29:8; 2 Nyak.10:8-13; 2 Fal.2:23-24. Kuhusu Juma la watoto Efe. 6:1-4; Isa. 54:13; Mith. 1:8-9; Zab. 127:3; Mat. 19:13-14; Mith. 17:6; 3Yoh 1:4; Kumb. 5:29; Mat. 18:13; Jer. Yn 6:9; Mith. 10:1; Kol. 3:20; Kut. 20:12; Mdo. 16:31; Mdo. 2:39; 1 Kor. 7:14-15; 2 Nyak. 34:1-3.

91

Kielelezo A. Mpangilio wa Mkao Kanisani

92